logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Timu za Uingereza zapata taabu kwenye ligi ya mabingwa barani Ulaya

Man City, Aston Villa na Arsenal walipoteza mechi za raundi ya pili ugenini Jumanne na Jumatano

image
na Brandon Asiema

Football07 November 2024 - 09:43

Muhtasari


  • Liverpool inaongoza msimamo wa jedwali wa ligi ya mabingwa baada ya kushinda mechi zote nne ikibakisha mechi nne kufuzu moja moja kwa hatua ya mbeleni.
  • Aston Villa na Arsenal walifungwa bao moja kila mmoja Jumatano usiku na Club Brugge na Inter Milan mtawalia kupitia mikwaju ya penalti.

caption

Mkondo wa nne wa michuano ya klabu bingwa barani Ulaya umekuwa mzito kwa timu za Uingereza baada ya matokeo ya kutoridhisha kurekodiwa Jumanne na Jumatano usiku.


Uingereza inawakilishwa na timu za Liverpool, Manchester City, Aston Villa na Arsenal  na kati ya timu hizi, ni Liverpool pekee iliyovuna ushindi katika mechi za mkondo wa nne kwenye ligi hiyo.


Jumanne usiku, mabingwa mara nne mfululizo wa ligi ya Uingereza Manchester City walipoteza kwa Sporting CP mabao manne kwa moja ugenini huku Liverpool wakiandikisha ushindi muhimu wa mabao manne kwa nunge dhidi ya Bayer Leverkusen ya Ujerumani.


Ugumu kwa timu za Uingereza kuandikisha matokeo mazuri yaliendelea Jumatano uaiku huku wakati Aston Villa na Arsenal wakipoteza kwa kunyoroshwa bao moja kwa kavu kila mmoja.


Club Brugge ikiwa nyumbani iliilambisha vumbi Aston Villa kupitia bao la mchezaji Hans Vanaken la penalti katika dakika ya 52 ya mchezo. Masaibu ya Arsenal yaliwapata dakika za nyongeza kabla ya mapumziko kwa Inter Milan kupata penalti baada ya mpirfa kumpiga Mikel Merino mkononi.


Kufikia sasa, ikiwa inasalia mechi nne za kubaini timu zitakazofuzu moja kwa moja kwa hatua inayofuata kwa kumaliza katika nane bora, Liverpool inashikilia nafasi ya kwanza kwa alama 12 baada ya ushindi wa mechi zote nne ikiimarisha fursa ya kufuzu moja kwa moja.


Aston Villa ipo katika nafasi ya nane kwa alama tisa baada ya kupoteza mechi moja dhidi ya Club Brugge Jumatano usiku.


Man City na Arsenal wanashikilia nafasi ya 10 na 12 mtawalia kwa alama saba kila mmoja na ikiwa watamaliza katika na nafasi kati ya 9 na 24, watalazimika kucheza mechi za maondoano moja ya nyumbani na nyingine ya ugenini ili kufuzu hatua ya mbele.



RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved