
Klabu ya Southampton imeweka historia isiyotakiwa kwenye Ligi Kuu ya Uingereza baada ya kushushwa daraja huku zikiwa zimesalia mechi saba za msimu.
Hii ni baada ya kupokea kichapo cha mabao 3-1 kutoka kwa Tottenham Hotspur katika mchezo uliochezwa Jumapili, Aprili 6, 2025 — na hivyo kuwa timu ya kwanza katika historia ya Premier League kushushwa daraja mapema kiasi hicho katika msimu wa mechi 38.
Rekodi ya awali ya kushushwa daraja mapema ilikuwa inashikiliwa na Derby County (msimu wa 2007-08) na Huddersfield Town (2018-19), ambao wote waliteremka daraja wakiwa na mechi sita mkononi. Kwa sasa, Southampton ndiyo wanaoshikilia rekodi hiyo peke yao.
Msimu huu umekuwa wa majonzi kwa Southampton. Baada ya mechi 31, wamekusanya pointi 10 pekee na bado wanahitaji angalau pointi mbili zaidi ili kuepuka kuwa na rekodi mbaya zaidi ya kihistoria ya Derby County, waliomaliza msimu na pointi 11. Kwa kuwa Wolves wako pointi 12 juu yao katika nafasi ya 17, matumaini ya kubaki kwenye ligi yalikatika rasmi Jumapili.
Matatizo ya Southampton yalianza mapema msimu huu, wakipoteza mechi nane kati ya tisa za kwanza na kushindwa kushinda yoyote kati ya mechi 12 za mwanzo.
Kocha Russell Martin alifutwa kazi mwezi Desemba akiwa amepata pointi tano pekee. Simon Rusk alichukua kwa muda mfupi kabla ya Ivan Juric kuteuliwa. Hata hivyo, Juric pia ameambulia ushindi mmoja tu katika mechi 14 za ligi.
Kwa sasa, Southampton ndiyo timu yenye safu ya ushambuliaji dhaifu zaidi kwenye ligi zote kuu za England, wakiwa wamefunga mabao 23 pekee. Pia wana ulinzi mbovu zaidi, wakiwa wamefungwa mabao 74 — idadi kubwa zaidi ya magoli katika EPL msimu huu.
Vilevile, wamepoteza mechi 25 kati ya 31, sawa na rekodi mbaya za Sunderland (2005-06) na Sheffield United (2020-21).
Akizungumza baada ya kushushwa daraja, Juric alisema: “Mashabiki wanastahili zaidi. Ni wakati wa kutafakari makosa yetu na kuanza kujenga kitu imara.”
Kipa Aaron Ramsdale, anayekumbana na kushuka daraja kwa mara ya tatu baada ya Bournemouth (2019-20) na Sheffield United (2020-21), alisema: “Hatupaswi kuwa na rekodi hiyo. Tutapambana kupata pointi zaidi.”
Naye nahodha Jan Bednarek alisema: “Hatuwezi kubadili yaliyopita. Kilichobaki ni kujifunza, kujiboresha na kujiandaa kujenga kitu bora zaidi.”
Kwa sasa, Southampton wamebakiwa na lengo moja tu — kujaribu
kuepuka kuwa timu mbaya zaidi katika historia ya Premier League.