Hatimaye EPL yarejea; Fahamu mambo ya kuangaziwa zaidi katika wiki ya nne ya Ligi Kuu

Muhtasari

•Baadhi ya wachezaji wapya ambao walinunuliwa siku za mwisho za dirisha la uhamisho wanatazamiwa kushiriki mechi zao za kwanza na klabu zao mpya.

•Liverpool, Manchester United, Manchester City, Chelsea na Leeds zitakosa huduma za Alisson Becker, Fabinho, Roberto Firmino, Fred, Ederson, Gabriel Jesus, Thiago Silva na Raphinha ambao wamepigwa marufuku ya kushiriki mechi kwa siku tano na FIFA kwa kukosa kuwakilisha mataifa yao wakati wa michuano ya kuhitimu kucheza kombe la Dunia.

Image: HISANI

Hatimaye Ligi kuu Uingereza (EPL) imerejea baada ya kipindi cha wiki mbili cha mapumziko ya kimataifa.

Jedwali la EPL limatazamiwa kuanza kuchukua sura huku mashindano hayo yakiingia wiki ya nne.

Kwa sasa Tottenham, West Ham, Manchester United na Chelsea zinashikilia nafasi ya 1,2,3 na 4 mtawalia huku Wolves, Norwich na Arsenal zikishikilia nafasi tatu za mwisho mtawalia bila pointi yeyote kutoka kwa mechi tatu ambazo tarari zimechezwa.

Jumla ya mechi nane zinatazamiwa kuchezwa siku ya Jumamosi huku mechi kati ya Crystal Palace na Tottenham ikifungua rasmi wiki ya nne ya EPL mida ya saa nane unusu.

Mechi sita zitakuwa zinaendelea mida ya saa kumi na Moja, mechi kubwa ikiwa kati ya washindi wa kombe la FA msimu uliopita Leicester City dhidi ya washindi wa EPL 2020 Manchester City.  Mechi hiyo itachezewa ugani King Power.

Arsenal ambayo imeshika mkia itakaribisha Norwich ambayo imeshikilia nafasi ya 19 ugani Emirates, United wakaribishe Newcastle ugani Old Trafford, West Ham watakuwa wageni wa Southampton, Watford wacheze dhidi ya Wolves huku Brighton wakitembelea Brentford  ugani Brentford Community Stadium.

Mechi ya mwisho siku ya Jumamosi itakuwa kati ya Chelsea na Aston Villa ambayo itachezwa mida ya saa moja unusu usiku, masaa ya Afrika Mashariki uwanjani Stamford Bridge.

Mechi moja tu kati ya Liverpool na Leeds itachezwa siku ya Jumapili mida ya saa kumi na mbili jioni ugani Elland Road.

Mechi ya mwisho ya wiki ya nne itakuwa kati ya Everton na Burnley ambayo itachezwa mida ya saa nne usiku wa Jumatatu .

Baadhi ya wachezaji wapya ambao walinunuliwa siku za mwisho za dirisha la uhamisho wanatazamiwa kushiriki mechi zao za kwanza na klabu zao mpya.

Miongoni mwa wachezaji ambao wanaangaziwa sana ni pamoja na mshambuliaji nyota Christiano Ronaldo ambaye alirejea United, mlinzi Takehiro Tomoyasu aliyesajiliwa na Arsenal, kiungo wa kati  Saul Niguez ambaye  alichukuliwa na Chelsea kwa mkopo kutoka Atletico Madrid na mlinzi Emerson Loyal ambaye alisajiliwa na Tottenham kutoka Barcelona.

Liverpool, Manchester United, Manchester City, Chelsea na Leeds zitakosa huduma za Alisson Becker, Fabinho, Roberto Firmino, Fred, Ederson, Gabriel Jesus, Thiago Silva na Raphinha ambao wamepigwa marufuku ya kushiriki mechi kwa siku tano na FIFA kwa kukosa kuwakilisha mataifa yao wakati wa michuano ya kuhitimu kucheza kombe la Dunia.

Arsenal itakosa huduma za kiungo wake muhimu Granit Xhaka ambaye alionyeshwa kadi nyekundu walipokuwa wanacheza dhidi ya Manchester City huku Chelsea ikimkosa beki Recce James ambaye alipokea kadi nyekundu wakicheza na Liverpool.