Barca yatangaza Xavi kama kocha mpya miaka sita baada yake kuondoka

Muhtasari

•Barca imetangaza kwamba Xavi atawasili mjini Barcelona siku ya Jumatatu na kutambulishwa kama kocha mpya katika hafla itakayofanywa hadharani ugani Camp Nou.

•Xavi anachukua  unachukua usukani wakati klabu hiyo ikiwa imekalia nafasi ya tisa baada ya kuandikisha pointi 16 tu katika mechi 11 zilizochezwa tayari.

Image: INSTAGRAM// XAVI

Klabu ya Barcelona imetangaza usajili wa kocha mpya Xavi Hernandez.

Xavi ambaye ni mchezaji wa zamani wa klabu hiyo atajaza nafasi iliyoachwa baada ya kocha Ronald Koeman kupigwa kalamu mwishoni mwa  mwezi Oktoba kufuatia msururu wa matokeo mabaya.

Rais wa Barcelona Joan Laporta alifahamisha Koeman kuhusu uamuzi wa bodi wa kumuachisha kazi punde baada ya miamba hao wa soka nchini Uhispania kupoteza ugenini dhidi ya Rayo Vallecano mnamo Oktoba 27.

Xavi anarejea Barcelona miaka sita baada yake kuondoka pale kuelekea Al-Sadd angali akiwa mchezaji.

Kiungo huyo wa kati wa zamani alichukua uongozi wa Al-Sadd kama mkufunzi baada ya kustaafu 2019 na tangu wakati huo amesaidia klabu hiyo kuandikisha matokeo bora na hata kushinda ligi ya Qatar msimu uliopita.

Barca imetangaza kwamba Xavi atawasili mjini Barcelona siku ya Jumatatu na kutambulishwa kama kocha mpya katika hafla itakayofanywa hadharani ugani Camp Nou.

Xavi ataongoza  miamba hao wa soka nchini Uhispania katika kipindi cha msimu huu kilichosalia na kuendelea kwa misimu ingine miwili.

Anachukua  unachukua usukani wakati klabu hiyo ikiwa imekalia nafasi ya tisa baada ya kuandikisha pointi 16 tu katika mechi 11 zilizochezwa tayari.