Mchezaji wa Simba agoma kuomba radhi

Muhtasari

• Mshambuliaji matata wa timu ya Simba nchini Tanzania, Mghana Bernard Morrison amegoma kuandika barua ya maelezo kwa timu hiyo

• Morrison alituhumiwa kukosa nidhani akiwa kambini na uongozi wa timu hiyo ukafikia uamuzi wa kumsimamisha kwa muda

Bernard Morrison
Image: Simba SC (Facebook)

Mshambuliaji matata wa timu ya Simba nchini Tanzania, Mghana Bernard Morrison amegoma kuandika barua ya maelezo kwa timu hiyo kama alivyoagizwa mwishoni mwa wiki jana alipofurushwa katika kambi ya timu hiyo kwa tuhuma za kinidhamu.

Morrison ambaye amekuwa katika fomu nzuri kwa mechi za timu ya Simba alituhumiwa kukosa nidhani akiwa kambini na uongozi wa timu hiyo ukafikia uamuzi wa kumsimamisha kwa muda ili kukamilisha uchunguzi dhidi ya nidhamu yake.

Baadae Morrison alitakiwa kuandika barua ya maelezo kwa ofisi ya mtendaji mkuu wa timu hiyo Barbara ila yeye amegomea hatua hiyo na kusisitiza kwamba hana hatia yeyote na haoni haja ya kuandika barua ya aina yoyote na kwa gharama yoyote ile.

Baadhi ya uongozi wa Simba unataka timu hiyo kukatisha mkataba na winga huyo wa Ghana huku timu hiyo ikidhibitisha kutopokea barua ya Morrison kama walivyokuwa wamesubiria.

Taarifa kutoka kwa ofisi ya msemaji wa timu ya Simba Ahmed Ally inasema klabu ingali kupokea barua au taarifa zozote kutoka kwa mchezaji huyo.