Ronaldo ndiye chanzo cha kufutwa kwa Tuchel, kivipi?

Tuchel alikataa kumsajili Ronaldo kuja Chelsea jambo lililozua mkwaruzano baina yake na wmiliki wa klabu.

Muhtasari

• Wamiliki wapya wa klabu ya Chelsea waliweka wazi mara kadhaa kwamba walikuwa wanamtaka Ronaldo

Christiano Ronaldo ndiye alisababisha kufutwa kwa Tuchel
Christiano Ronaldo ndiye alisababisha kufutwa kwa Tuchel
Image: Instagram, Maktaba

Mapema wiki hii, klabu ya Chelsea nchini Uingereza ilimfuta kazi aliyekuwa kocha mkuu Thomas Tuchel, saa chache baada ya kudhalilishwa na malimbukeni kutoka Croatia, Dyanmo Zagreb.

Wengi waliamini kabisa kwamba kichapo hicho katika ufunguzi wa kampeni za kipute cha klabu bingwa ulaya ndiyo sababu kubwa ya Tuchel kuoneshwa mlango.

Ila zogo limekolea zaidi baada ya baadhi ya majarida nchini Uingereza kuripoti kwamba kupoteza dhidi ya Zagreb halikuwa tukio kubwa bali kufutwa kazi kwake kulikuwa kumejadiliwa na kupangwa awali na wamiliki wa klabu hiyo.

Jarida la Football London lilisema kwamba Tuchel alifutwa kazi baada ya kukataa kumsajili mchezaji wa Manchester United, Christiano Ronaldo wakati wa kipindi cha joto uhamisho wa wachezaji ambacho kimekamilika juzi.

Wamiliki wapya wa klabu ya Chelsea waliweka wazi mara kadhaa kwamba walikuwa wanamtaka Ronaldo kuisakatia timu hiyo ila kocha Tuchel aliarifiwa kukataa kwa madai kwamba mchezaji huyo atavuruga kikosi chake.

“Todd Boehly amekubali kila kitu kumsajili Cristiano Ronaldo, lakini Thomas Tuchel alimtanguliza Aubameyang. Jambo hilo hilo lilifanyika kwa Jules Koundé, ambaye alichagua FC Barcelona badala ya Chelsea,” Football London walinukuu jarida la Managing Barca kweney Twitter na kusema mkwaruzano huo baina ya mmiliki wa kocha ndio ulisababisha kibarua cha kocha Tuchel kuota nyasi na magugu.

Baada ya kumfuta kazi kocha Tuchel, Chelsea siku mbili baadae walitangaza kumuandika kazi kocha wa Brighton & Hoven, Graham Potter, siku moja tu kabla ya ligi ya EPL kusitishwa kutokana na kifo cha malkia Elizabeth wa pili wa Uingereza.