Victor Wanyama akanusha uwezekano wa kurejea Tottenham

Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 31 alihamia Montreal mnamo Machi 2020 baada ya kuachiliwa na Spurs.

Muhtasari
  • Mapema Oktoba, Wanyama alitangaza kuwa hataongeza mkataba wake na CF Montreal mwishoni mwa msimu
  • Mkataba wa sasa wa Wanyama na timu hiyo ya Ligi Kuu ya Kanada unamalizika mwishoni mwa mwaka huu
VICTOR WANYAMA
Image: KWA HISANI

Mwanasoka wa Kenya na nahodha wa zamani Victor Wanyama amekana uwezekano wa kurejea Tottenham Hotspur.

Katika mahojiano na kituo cha BBC Africa Focus, Wanyama alisema ziara yake katika klabu hiyo ya soka ilikuwa ni kusalimia tu watu aliowaacha hapo.

Wanyama anayechezea CF Montreal aliongeza kuwa ana marafiki na familia huko London, ndiyo maana anatembelea mara kwa mara.

"London pia ni nyumbani kwangu. Huwa napitia kuwasalimia marafiki. Nina familia hapa," alisema.

Kuhusu kama kurejea kwake katika klabu ilikuwa ni ishara ya kurejea, alisema, "Si kweli. Hiyo ilikuwa kama kurudi kusalimia watu, kwani kila mtu anajua spurs ni kama familia kwangu."

Wikendi ya kwanza ya Novemba, nahodha huyo wa zamani wa Harambee Stars alishiriki picha zake na mkewe na mwana wao katika uwanja wa Tottenham Hotspur.

Picha hizo zilichukuliwa sana kuwa yeye akidokeza uwezekano wa kurejea klabuni.

Mapema Oktoba, Wanyama alitangaza kuwa hataongeza mkataba wake na CF Montreal mwishoni mwa msimu.

Mkataba wa sasa wa Wanyama na timu hiyo ya Ligi Kuu ya Kanada unamalizika mwishoni mwa mwaka huu.

"Kusema kweli, nadhani swali hili limeulizwa kwa muda mrefu na ukweli ni kwamba mwisho wa msimu nitaondoka. Nilikuwa na miaka nzuri hapa, nilifurahia kuwa sehemu ya timu. Imekuwa nzuri," alisema.

“Mwisho wa msimu nitakuwa huru kuondoka, lakini muda wote nikiwa hapa nitaendelea kuwa makini na kuhakikisha kwamba tunamaliza vizuri na nikitoka hapo nitapata nafasi ya kuaga.”

Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 31 alihamia Montreal mnamo Machi 2020 baada ya kuachiliwa na Spurs.

Hapo awali amecheza katika klabu za Germinal Beerschot AC, Celtic na Southampton FC.