Ronaldo na Messi wazika uhasama wao, washiriki mchezo wa Chess pamoja

Kwa zaidi ya miaka 16, wawili hao wamekuwa wakisemwa kuwa na uhasama kutokana na kila mmoja kutaka kutajwa kama mfalme wa soka katika karne hii.

Muhtasari

• “Ushindi ni hali ya akili. Tamaduni ndefu ya kutengeneza vigogo,” Ronaldo na Messi waliandika kwenye akaunti zao mitandaoni.

Ronaldo na Messi kwa mara ya kwanza wakutana kwenye mchezo wa Chess
Ronaldo na Messi kwa mara ya kwanza wakutana kwenye mchezo wa Chess
Image: Twitter

Masupastaa maarufu wa mchezo wa kandanda Duniani Christiano Ronaldo na Lionel Messi kwa mara ya kwanza wameonekana wakiwa pamoja wakishiriki mchezo wa chess huku wakisubiria kuwajibikia mataifa yao katika kombe la dunia ambalo litang’oa nanga Novemba 20 huko Qatar.

Katika picha hiyo ambayo Ronaldo aliipakia kwenye mitandao yake ya kijamii, wawili hao wanaonekana wameketi huku kila mmoja akipiga tathmini ya jinsi ya kucheza mchezo huo wa chess, picha ambayo imewafurahisha wengi wa mashabiki wa kandanda na haswa wale ambao kwa miongo zaidi ya miwili wamekuwa wakiendeleza gumzo kuhusu ni nani bora kati ya Mreno Ronaldo na Muargentina Messi.

Wawili hao wanaonekana kila mmoja akifikiria pakubwa jinsi ya kucheza mchezo huo huku Ronaldo akiachia maandishi kuwa mtu ukitaka kuibuka mshindi basi ni sharti ushirikishe akili na fikira zako kwenye kile unachokifanya.

“Ushindi ni hali ya akili. Tamaduni ndefu ya kutengeneza vigogo,” Ronaldo aliandika kwenye Twitter.

Kwa upande wake, Messi vile vile alinukuu maneno yay ohayo na kuwaacha mashabiki wao kufurahia kwa kuona hatimaye wawili hao ambao wamekuwa wakichukuliwa kuwa mahasimu wanaweza kiuka dhana hiyo na kushiriki muda wao wa mapumziko pamoja.

“Hii ni picha ya karne,” mmoja alisema.

“Ronaldo nimefurahi kukuona katika picha ya pamoja na Messi, lakini natumai onyesho hili la upendo !sio la kiki,” Daniel Regha aliwasifia.

“Mabao 1604 bila mechi za kirafiki, vikombe 75, 12 ballon'dor, vyote katika picha moja….picha nzito zaidi katika historia ya soka 🐐🐐” mwingine aliandika.

Juzi katika mahojiano ya kipekee na mwanahabari mwenye utata, Piers Morgan, Ronaldo aliulizwa jinsi atakavyohisi endapo watakutana na Messi kwenye fainali za kombe la dunia nchini Qatar na kusema kwamba endapo hilo litatokea basi itakuwa ni moja ya ndoto nzuri sana katika maisha yake.

Pia alimzungumzia Messi na kusema kwamba ni mchezaji mzuri anayefanya kila jema awezalo kwa ajili ya mchezo wa kandanda, na pia kumsifia kwa jinsi anavyomzungumzia vizuri kila mara katika mahojiano.

Alisema yeye na Muargentina huyo ni marafiki wakubwa, si tu wao pekee bali hata wapenzi wao ambao wote wanatoka taifa la Argentina.