Wachezaji wa Uhispania waruhusiwa kufanya mapenzi usiku mmoja kabla ya mechi

Kocha mkuu Luis Enrique alisema kuwa hakuna ubaya wachezaji kushiriki mapenzi na wapenzi wao usiku kabla ya mechi kwani ni jambo la kawaida mno.

Muhtasari

• Ninapokuwa mkufunzi wa klabu wachezaji huwa nyumbani usiku wa kuamkia mchezo na si jambo linalonitia wasiwasi hata kidogo - Enrique alinukuliwa na majarida.

Kikosi cha kwanza cha Uhispania
Kikosi cha kwanza cha Uhispania
Image: Getty Images

Kocha mkuu wa timu ya taifa ya Uhispania Luis Enrique ameweka wazi kwamba anawaruhusu wachezaji wake kushiriki mapenzi na wapenzi wao kabla ya mechi.

“Sijali wachezaji wakifanya tendo la ndoa usiku wa kuamkia mechi lakini ninaweka mstari kwenye karamu,” alisema kocha wa Uhispania Luis Enrique katika mtiririko wake wa hivi punde kwa mashabiki kutoka Qatar.

Meneja huyo wa Uhispania pia alikiri angependa kuhamia Uingereza katika siku zake za kucheza akiongeza uvumi kwamba ataishia kufundisha klabu moja katika Ligi ya Premia siku moja.

Kocha huyo asiye wa kawaida alikuwa akizungumza kwenye Twitch, akitimiza ahadi yake kwa mashabiki ya kuendelea kutiririka kwa muda wote Uhispania ikiwa kwenye Kombe la Dunia.

Alipoulizwa pia ikiwa wachezaji wanapaswa kuambiwa wasifanye mapenzi kabla ya michezo alisema: “Ni ujinga (kuipiga marufuku). Ni kitu ninachokiona cha kawaida kabisa. Ikiwa uko kwenye tafrija usiku mmoja kabla ya mechi basi ni wazi hilo si jambo zuri, lakini ninapokuwa mkufunzi wa klabu wachezaji huwa nyumbani usiku wa kuamkia mchezo na si jambo linalonitia wasiwasi hata kidogo.”

“Ikiwa ni kitu wanachofanya basi ni kwa sababu wanahitaji na wanataka. Lakini narudia kwa akili ya kawaida! Kila mmoja na mwenzake. Ni kawaida. Nilipokuwa mchezaji kama ningekuwa nyumbani kabla ya mchezo, na mke wangu, tulifanya kile tulichopaswa kufanya,” Enrique aliongezea.

Nyota wa Enrique katika kikosi chake cha Uhispania - Ferran Torres - kwa sasa anatoka kimapenzi na bintiye na hapo awali alitania kuwa 'atamkata kichwa' ni endapo angeshindwa kumwanzisha kwenye mchezo.

Siku mbili zilizopita, timu ya taifa ya Uhispania ilishiriki mechi yao ya kwanza kufungua kampeni zao kutafuta ubingwa wa kombe la dunia ambapo iliititiga Costa Rica mabao 7 bila jibu.

Baada ya mechi hiyo iliyoonyesha ubora wao, Uhispania inapigiwa upato mkubwa katika mashindano hayo huku wengi wakisema huenda itakuwa timu ya kutazamwa kwa umakini.

Jumapili, Uhispania watashuka dimbani kumenyana na Ujerumani katika mechi inayotajwa kuwa ya moto kuamua hatma ya Ujerumani katika mashindano hayo.

Uhispania ni mabingwa wa kombe la dunia la mwaka 2010 lililoandaliwa nchini Afrika Kusini.