Ronaldo atamalizia taalum yake ya soka Yanga - Haji Manara

Manara ambaye alikuwa msemaji wa Yanga kabla ya kupigwa marufuku na TFF alisema walikutana na Ronado Qatar na akampa hakikisho hilo.

Aliyekuwa msemaji wa timu ya soka nchini Tanzania HajiManara ameibua gumzo mitandaoni baada ya kudai kwamba alikutana na staa wa Ureno Christiano Ronaldo nchini Qatar na wakawa na maongezi ya kina.

Manara alifadhiliwa safari ya kwenda Qatar na kampuni ya michezo ya Kamari ya Wasafi Bet na aliongozana na  wake zake wawili kushuhudia mechi ya kufuzu hatua ya 16 bora kombe la dunia ambazo zinaendelea kuchezwa katika viwanja mbalimbali Qatar.

Alipakia video akiwa pamoja na wake zake na kuifuatisha kwa maneno ya kuwatia moyo sana wapenzi wa Yanga baada ya kusema kuwa mwamba Ronaldo alimdokezea ana hamu ya kuja kumaliza taaluma yake ya soka nchini Tanzania akichezea mabingwa hao wa ligi kuu ya NBC nchini Tanzania – Yanga SC.

Tumeamka salama salmini Alhamdulillah,,,,,na salaam zenu toka Kwa @cristiano ,,kaniambia mida hii kwenye breakfast,,hamu yake ni kuja kumalizia Soka lake Yanga Afrikaaaaaaa,” Manara aliandika.

Wengi walichukulia kauli hizo kwa kizembe huku baadhi wakisema kuwa lolote linawezekana katika ulimwengu wa soka.

Ronaldo amekuwa akihusishwa na vilabu mbalimbali tangu klabu ya Manchester United kutangaza wiki mbili zilizopita kuwa wamefikia makubaliano na mchezaji huyo kusitisha mkataba wake na kuondoka mara moja.

Kuondoka kwa Ronaldo Manchester kulichochewa na mahojiano ya moto aliyoshiriki na mwanahabari mwenye utata Pier Morgan ambapo alifunguka kwa kiasi cha haja jinsi maisha yake yamekuwa katika klabu hiyo kwa misimu miwili tangu kurejea akitokea Juventus ya Italia.

Alipasua mbarika kuwa kamwe hawezi kuwa na heshima kwa kocha mkuu Eric Ten Hag kwa kile alitaja kuwa mkufunzi huyo alimuonesha dharahu na kebehi. Pia alisema klabu hiyo imesalia nyuma kiteknolojia, matamshi ambayo yalionekana kuwaguza vikali baadhi ya watu wa klabu hiyo kupelekea uamuzi wa kukatisha mkataba wake.

Huku akiendelea kulitumikia taifa lake la Ureno katika mashindano ya Kombe la dunia, Ronaldo amekuwa akihusishwa na vilabu mbali mbali huku tetesi za hivi karibuni zikimhusisha na kujiunga na klabu moja ya Saudi Arabia kwa posho nono ajabu.

Ronaldo mwenye umri wa miaka 37 alisema kuwa anatarajia kucheza katika viwango vya juu zaidi kwa takribani miaka mitatu ijayo na pindi atakapofikisha umri wa miaka 40, atastaabu kucheza soka.