Kocha Antonio Conte kufanyiwa upasuaji wa kutolewa nyongo baada ya kuugua

Konte ameratibiwa kufanyiwa utaratibu huo hivi leo, Februari 1.

Muhtasari

•Tottebham ilifichua kwamba Conte hivi majuzi alikumbwa na maumivu makali ya tumbo ambayo yalimlazimu kutafuta huduma za matibabu.

•Spurs walimtakia mkufunzi huyo afueni ya haraka huku wakitazamia kurejea kwake ili awaongoze katika kuwinda taji la EPL.

Kocha Antonio Conte
Image: TWITTER// ANTONIO CONTE

Klabu ya Tottenham Hotspurs itazikosa huduma za kocha wake Antonio Conte kwa muda usiojulikana baada ya raia huyo wa Italia kuugua.

Siku ya Jumatano alasiri, klabu hiyo ya jiji la London ilifichua kwamba Conte hivi majuzi alikumbwa na maumivu makali ya tumbo ambayo yalimlazimu kutafuta huduma za matibabu.

Baada ya vipimo kadhaa, ilipendekezwa afanyiwe upasuaji wa kuondoa kibofu cha nyongo na anatarajiwa kufanyiwa utaratibu huo hivi leo, Februari 1.

"Antonio Conte hivi majuzi aliugua kwa maumivu makali ya tumbo. Kufuatia kugundulika kwa ugonjwa wa cholecystitis, atafanyiwa upasuaji wa kuondoa kibofu cha nyongo leo na atarejea kufuatia muda wa kupona," Taarifa ya Tottenham ilisoma.

Spurs walimtakia mkufunzi huyo afueni ya haraka huku wakitazamia kurejea kwake ili awaongoze katika kuwinda taji la EPL.

Bado haijabainika Conte atakosa mechi ngapi za Tottenham. Klabu hiyo inatazamiwa kumenyana na mabingwa watetezi wa Ligi Kuu, Manchester City siku ya Jumapili kabla ya kusafiri hadi Leicester wikendi ifuatayo.

Conte alikuwa dimbani siku ya Jumamosi iliyopita wakati timu yake ya Tottenham ilipata ushindi wa mabao 3-0 katika mechi ya raundi ya nne ya Kombe la FA dhidi ya Preston North End.