"Ni upuzi kusema tulikata tamaa!" Rashford azungumzia kichapo ya 7-0 dhid ya Liverpool

Kilichotokea ni kwamba tulipoteza mawasiliano uwanjani, na hiyo ndio sababu tuliona ugumu.

Muhtasari

• Tulipotoka nje ya falsafa ya timu na umiliki wa mchezo.

Rashford akanusha United kukata tamaa.
Rashford akanusha United kukata tamaa.
Image: Twitter

Mshambuliaji wa Manchester United, Muingereza Marcus Rashford amezungumza kwa mara ya kwanza kuhusu matokeo ya kudhalilisha ambayo timu yake ilipokea mikononi mwa Liverpool wikendi iliyopita.

Akizungumza na wanahabari saa chache kuelekea maandalizi ya mechi ya ligi ya Uropa dhidi ya Real Betis, Rashford alipuuzilia mbali vikali madai na minong’ono mitandaoni kwamba wachezaji wa United walikata kata katika mechi hiyo ambayo Liverpool iliichabanga United kibano cha mabao 7 bila jibu.

Kulingana na mshambulizi huyo wa miaka 25, wachezaji wa United hawakukata tamaa, madai ambayo aliyataja kuwa ya kipuuzi.

“Hatukukata tamaa, huo ni upuzi, kilichotokea ni kwamba tulipoteza mawasiliano uwanjani, na hiyo ndio sababu tuliona ugumu wa kupenya kwenye lango la Liverpool. Tulipotoka nje ya falsafa ya timu na umiliki wa mchezo. Mimi naamini kwamba kila mtu alikuwa anajaribu kujitafuta na kujirudi kwenye mechi ile,” Rashford alisema.

Matokeo ya mechi hiyo yamekuwa gumzo kubwa mitandaoni kwa Zaidi ya siku tani tangu kufanyika usiku wa Jumapili na wadau mbali mbali wamekuwa wakitoa maoni yao kuhusu kulichojiri kwa washindi hao wa kombe la Carabao.

Bruno Fernandes amekuwa akikosolewa kwa mtazamo wake alipokuwa nahodha wa timu hiyo wikendi. Kiungo huyo wa kati wa Ureno amekuwa akiteuliwa mara kwa mara kuwa nahodha wa Ten Hag msimu huu huku nahodha wa klabu hiyo Harry Maguire akichemsha mahindi kwenye benchi.

Fernandes mara kwa mara aliwaadhibu wachezaji wenzake na hata kumsukuma mmoja wa wasaidizi wa mwamuzi katika kufadhaika kwake. Lakini Ten Hag alithibitisha kuwa atasalia nahodha wakati Maguire hatachaguliwa.