Harambee Stars yashinda mechi yao ya kwanza dhidi ya Pakistan

Moses Shumah alifunga bao lake la kwanza kwa timu ya Harambee Stars katika ushindi wa 1-0 wa Kenya dhidi ya Pakistan.

Muhtasari

• Kenya, ambayo ilikosa mchezo wao wa ufunguzi dhidi ya Djibouti siku ya Jumapili, itamenyana na wenyeji Mauritius.

• Shumah aliuwahi mpira ndani ya eneo la hatari na kufunga bao dakika ya 18 huku Engin Firat akianza shindano hilo la wiki moja kwa ushindi.

Image: HISANI

Timu ya taifa ya Harambee Stars siku ya Jumatano iliicharaza timu ya taifa ya Pakistan katika  mechi yake ya kwanza kwenye mchuano wa mataifa manne nchini Mauritius. 

Mshambuliaji wa Kakamega Homeboyz, Moses Shumah alifunga bao lake la kwanza kwa timu ya Harambee Stars katika ushindi wa 1-0.

Shumah aliuwahi mpira ndani ya eneo la hatari na kufunga bao dakika ya 18 huku Engin Firat akianza shindano hilo la wiki moja kwa ushindi.

Shumah, ambaye anajivunia mabao manne na kuchangia bao moja akiwa na Homeboyz katika Ligi Kuu ya Kenya (KPL) , aliitingisa wavu baada ya kumzunguka kipa wa Pakistan, Yousaf Butt na kuiweka Harambee Stars uongozini.

Stars ilitawala zaidi kipindi cha kwanza huku beki David 'Cheche' Ochieng akikaribia kupata bao la kuongoza kutoka kwa kona lakini kombora lake liliapaa juu ya mtambaa panya. 

Bashir Hassan wa Pakistan alikosa nafasi ya wazi ya kusawazisha baada ya kuuwahi mpira mzuri kutoka kwa krosi ya Sufyan Mohammed.

Pakistani walikuwa bora mwanzoni mwa kipindi cha pili na walitawala Stars lakini walishindwa kupata bao la kusawazisha.

Kenya, ambayo ilikosa mchezo wao wa ufunguzi dhidi ya Djibouti siku ya Jumapili, itamenyana na wenyeji Mauritius katika mechi ya pili.

Pakistan sasa wamepoteza mara mbili, baada ya kufungwa 3-0 na Mauritius siku ya Jumapili. Watamenyana na Djibouti katika mechi yao ya mwisho katika mchuano huo.