Rachier: Gor Mahia haitasajili wachezaji wa kigeni tena

"Inaonekana wachezaji wengi wa kigeni ambao tumekuwa tukiwasajili wanakuja tu hapa kutuletea matatizo na kuchukua pesa bila kutupatia thamani," Rachier alisema.

Muhtasari

• CAF lilibatilisha cheti cha leseni ya klabu ya Gor Mahia siku ya Ijumaa baada ya klabu hiyo kushindwa kutimiza makubaliano ya malipo na wachezaji watatu wa zamani.

• Rachier alisema timu hiyo ilifikia uamuzi huo baada ya uongozi wa Gor Mahia kufanya mkutano na kukubaliana kuwa wachezaji hao wa nje ya nchi hawaisaidii klabu hiyo.

Gor Mahia imesema kuwa haitasajili wachezaji kutoka nje ya nchi.
Gor Mahia imesema kuwa haitasajili wachezaji kutoka nje ya nchi.
Image: Facebook

Mabingwa wa ligi ya Kenya, Gor Mahia hawatasajili mchezaji yeyote wa kigeni siku zijazo, mwenyekiti wa klabu hiyo Ambrose Rachier alisema, baada ya kutimuliwa kutoka kwa Ligi ya Mabingwa ya CAF kwa kukiuka masharti ya kandarasi ya wachezaji.

Shirikisho la Soka barani Afrika (CAF) lilibatilisha cheti cha leseni ya klabu ya Gor Mahia siku ya Ijumaa baada ya klabu hiyo kushindwa kutimiza makubaliano ya malipo na wachezaji watatu wa zamani kutoka Burundi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na Mali.

Klabu hiyo sasa imetolewa nje ya michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika ambayo droo yake ya awali itafanyika mjini Cairo siku ya Jumanne.

Mwenyekiti wa Gor Mahia Ambrose Rachier alisema siku ya Jumapili klabu hiyo haitasajili wachezaji wowote wa kigeni kwa siku zijazo.

"Inaonekana wachezaji wengi wa kigeni ambao tumekuwa tukiwasajili wanakuja tu hapa kutuletea matatizo na kuchukua pesa bila kutupatia thamani," Rachier alisema.

Rachier alisema timu hiyo ilifikia uamuzi huo baada ya uongozi wa Gor Mahia kufanya mkutano na kukubaliana kuwa wachezaji hao wa nje ya nchi hawaisaidii klabu hiyo.

"Tumekuwa na majadiliano kama uongozi wa juu wa klabu, na kwa sasa hatutasajili mchezaji yeyote wa kigeni,"

Gor Mahia ilipigwa maruku yakusajili na Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa) mwaka wa 2021 baada ya mshambuliaji wa Kongo Sando Yangayay na kipa wa Mali Adama Keita kulalamikia kuvunjwa kwa kandarasi.

Hata hivyo, marufuku hiyo ya uhamisho iliondolewa mapema mwaka huu baada ya klabu hiyo kufikia makubaliano na wachezaji hao wawili kulipa deni lao lililosalia ifikapo Mei 31, hivyo kuruhusu mabingwa hao wa Kenya kushiriki mashindano ya vilabu ya CAF msimu huu.

Lakini Ijumaa Shirikisho la Soka la Kenya (FKF) lilitangaza kufutilia mbali cheti cha leseni ya klabu hiyo baada ya Gor Mahia kushindwa kulipa malipo hayo ndani ya muda uliowekwa na CAF.