Messi aeleza jinsi 'uadui' kati yake na CR7 ulimfaidi katika malimwengu ya kandanda

"Tulikaa kileleni kwa miaka kumi au kumi na tano, sina uhakika ni ngapi, na ilikuwa ngumu sana”. Messi alisema.

Muhtasari

• "Ilikuwa vigumu sana kuendelea katika kiwango hiki na nadhani lilikuwa jambo kubwa na kumbukumbu nzuri kwa kila mtu anayefurahia soka,” aliongeza.

Lionel Messi na Cristiano Ronaldo
Lionel Messi na Cristiano Ronaldo
Image: Instagram

Nahodha wa timu ya taifa ya soka ya Argentina Lionel Messi kwa mara nyingine tena ameelezea jinsi kile kinachotajwa kuwa uadui wa ushindani baina yake na Mreno Christiano Ronaldo ulivyomfanya kucheza soka lake katika viwango vya juu kwa muda mrefu.

Akizungumza baada ya kushinda tuzo ya Ballon d’Or kwa mara ya 8, Messi aliulizwa iwapo sasa kuibuka na ushindi huo, ikiwa ni mara tatu Zaidi ya Ronaldo ambaye ameishinda tuzo hiyo mara tano, ndiko kutakuwa kunamaliza mwisho wa ushindani wao.

Akijibu, Messi alisema kwamba anamshukuru Ronaldo kwa kumpa ushindani huo ambao kwa njia moja au nyingine ulimfanya kutia bidii na kuhakikisha anacheza soka safi katika viwango vya juu kwa Zaidi ya miaka 15 ya ushindani wao.

"Ilikuwa mashindano makubwa kati ya mabano. Kwa spoti, Cristiano alikuwa mzuri sana na nadhani tulifaidika kutoka kwa kila mmoja kwa sababu sisi sote tunashindana sana na pia anataka kushinda kila mtu na kila kitu,” Messi alisema.

Mchezaji huyo ambaye ameweka rekodi ya kuwa mwanasoka wa kwanza kushinda tuzo hiyo kwa mara nyingi Zaidi aliwataka mashabiki wote wa soka kutolichukulia suala la ushindani wao kuwa uadui kwani kilikuwa ni kipindi cha kuleta furaha na mbwembwe katika malimwengu ya soka – na walifanikisha hilo kwa muda mrefu.

"Nadhani kilikuwa kipindi kizuri sana kwetu na kwa wale wanaopenda soka kwa ujumla. Tulichofanya muda wote huu kinathaminiwa sana kwa sababu wanavyosema ni rahisi kufika kileleni lakini ni vigumu kubaki. Tulikaa kileleni kwa miaka kumi au kumi na tano, sina uhakika ni ngapi, na ilikuwa ngumu sana”.

"Ilikuwa vigumu sana kuendelea katika kiwango hiki na nadhani lilikuwa jambo kubwa na kumbukumbu nzuri kwa kila mtu anayefurahia soka,” aliongeza.

Awali tulifahamu kwamba Ronaldo aliweka alama ya like na hata kukomenti kwa emoji za kucheka katika moja ya klipu ambayo mwanahabari mmoja alikuwa anajaribu kukashifu ushindi wa Ballon d’Or kwa mara ya nane.