RIP! Aliyekuwa mshikilizi wa rekodi nyingi za dunia Henry Rono amefariki

Kilele cha taaluma ya kukimbia ya Rono kilikuwa msimu wa 1978.

Muhtasari

•Rono, 72, alifariki mwendo wa saa nne unusu asubuhi siku ya Alhamisi katika Hospitali ya Nairobi South alikokuwa amelazwa kwa muda wa siku 10 zilizopita.

•Alipostaafu, alifundisha riadha ya shule huko Albuquerque, New Mexico, kabla ya kurejea Kenya mnamo 2019.

Marehemu Henry Rono
Image: HISANI

Aliyekuwa mshikilizi wa rekodi nyingi za dunia Henry Rono amefariki dunia.

Rono, 72, alifariki mwendo wa saa nne unusu asubuhi siku ya Alhamisi katika Hospitali ya Nairobi South alikokuwa amelazwa kwa muda wa siku 10 zilizopita.

Kilele cha taaluma ya kukimbia ya Rono kilikuwa msimu wa 1978.

Katika siku 81 pekee, alivunja rekodi nne za dunia; mita 10,000 ambapo alitumia 27:22.5, 5000 kwa 13:08.4 mbio za mita 3000 kuruka viunzi 8:05.4 na 3000 kwa 7:32.1, mafanikio ambayo hayajaonekana tena katika historia ya mbio za masafa.

Alipunguza rekodi ya 10,000 kwa karibu sekunde nane, 5000 kwa 4.5, mbio za kuruka viunzi na 2.6, na 3000 kwa sekunde tatu.

Aliboresha rekodi ya dunia ya mita 5000 mwaka 1981 nchini Norway, ambapo alitumia saa 13:06.20.

Katika mwaka huo huo, alishinda dhahabu katika mbio za mita 3000 kuruka viunzi na maji na mita 5000 kwenye Michezo ya Jumuiya ya Madola huko Edmonton, Kanada.

Pia alishinda dhahabu katika Michezo ya All Africa mjini Algiers, Algeria, akishinda katika mbio za mita 3000 kuruka viunzi na mbio za mita 10,000 mtawalia.

Aling'ara katika mikutano ya NCAA na mikutano ya uwanjani nchini USA.

Mwanariadha huyo maarufu kama Nandi Warrior alikaa karibu miaka 40 nchini Marekani, baada ya kufika huko mwaka wa 1976 kwa udhamini wa Riadha katika Chuo Kikuu cha Washington State.

Alipostaafu, alifundisha riadha ya shule huko Albuquerque, New Mexico, kabla ya kurejea Kenya mnamo 2019.