Omalla ashinda tuzo ya mfungaji bora FKF 23/24 kwa kupachika magoli 19

Elvis Rupia alimpiku Omalla msimu uliopita kwa kufunga mabao 27 huku Omalla akimaliza na 26

Muhtasari

•Benson Omalla alifikisha  jumla ya mabao 19 kwenye ligi kuu ya FKF baada ya kupachika magoli mawili  Jumapili 23, dhidi ya Bidco United.

•Tito Okello na John Makwata walimaliza wa pili kwa magoli 16.

Mshambulizi wa Gor Mahia
Benson Omalla Mshambulizi wa Gor Mahia
Image: Hisani

Mshambulizi wa Gor Mahia Benson Omalla alitawazwa mfungaji bora wa ligi kuu ya  FKF siku ya mwisho baada ya kupachika jumla ya magoli 19.

Benson Omala alinyakua kiatu cha dhahabu cha ligi kuu ya FKF baada ya kufunga bao la pili muhimu katika kipindi cha kwanza dhidi ya Bidco United siku ya mwisho ya msimu,Juni 23,2024 kwenye ushindi wa 4-2.

Uchezaji huu mzuri ulihakikisha kwamba Omala anamaliza kileleni mwa chati ya wafungaji bora baada ya kukosa nafasi ya kwanza msimu jana.

Mabao yake mawili hio jana yalifikisha jumla ya magoli 19 na kuwashinda washindani wake wa karibu katika kinyang'anyiro kilichokisiwa kuwa  kali.Tito Okello wa Kenya Police alimaliza wa pili kwa mabao 16 sawia  na John Makwata .

Mafanikio ya Omala yaliashiria wakati muhimu kwa Gor Mahia klabu hiyo ilipomaliza ligi ikiwa na pointi 73, uboreshaji mkubwa kutoka kwa kumaliza kwa pointi 70 msimu uliopita.

Mwaka jana, aliyekuwa mshambulizi wa AFC Leopards ,Elvis Rupia aliweka rekodi mpya akiwa na mabao 27, na kuipita rekodi ya miaka 47 kwa bao moja, huku Omala akimaliza na 26. Msimu huu umeshuhudia kudorora kwa ufungaji wa jumla ikilinganishwa na msimu wa 2022/23.

Aidha kipa wa Gor Mahia, Kevin Omondi alishinda glavu ya dhahabu mapema wiki chache zilizopita ,zikiwa zimesalia mechi 4 kabla ya ligi kutamatika.