Ten Hag adai kuboresha zaidi kikosi cha Manchester United

Mkufunzi huyo ametaja kuwa majeraha yalichangia pakubwa klabu yake kumaliza nafasi ya nane msimu uliopita.

Muhtasari

•Ten Hag amedai kuwa kikosi cha  Manchester United kina wachezaji wachache ukilinganisha na vilabu vingine.

•United imekuwa ikifanya usajili wa kupendeza baada ya kumsajili mshambulizi Zirkzee,beki Leny Yoro na ipo kwenye harakati za kuchukua Manuel Ugarte.

Kocha wa Man Utd Eric Ten Hag
Image: Hisani

Kocha mkuu wa klabu ya Manchester United,Eric ten Hag amedokeza kuwa bado yupo katika harakati za kujenga kikosi chake.

Raia huyo wa Uholanzi  amesema kuwa kikosi chake kina wachezaji wachache ukilinganisha na timu zingine huku akilaumu majeraha kwa kumaliza katika nafasi ya nane msimu uliopita.

Ten Hag mapema mwezi huu aliongeza kandarasi yake hadi 2026 licha ya uvumi kwamba angeondoka  baada ya msimu mbaya kando na kushinda kombe la FA mwishoni mwa kampeni.

Kwenye mazungumzo Ijumaa na gazeti la kila siku la Uholanzi Algemeen Dagblad, Ten Hag alitaja jumla ya mechi 61 za klabu yake katika mashindano yote msimu uliopita kuwa "za ajabu tu".

“Sisi sio timu pekee iliyokabiliwa na majeraha, vilabu vingine vilikuwa na hali kama hiyo. Msimu uliopita tulikuwa na majeruhi mara kwa mara kwa wachezaji katika nafasi sawa, wote nyuma. Wakati fulani tulikuwa karibu hakuna mabeki."

Aliongeza; "Nilipoanza hapa, United ilikuwa haijashinda kombe kwa miaka sita na haikuwa hivyo kwa sababu hawakuwa na wasimamizi wazuri hapa. Hii ina maana kuwa  utunzi na ubora wa kikundi cha wachezaji unachangia pakubwa."

United imekuwa ikifanya usajili wa kupendeza baada ya  kumsajili beki chipukizi wa Ufaransa ,Leny Yoro, kutoka Lille OSC.Beki huyo wa Ufaransa ametia saini kandarasi hadi Juni 2029, akiwa na chaguo la kuongeza mwaka mmoja zaidi.

Kwa sasa wapo katika harakati ya kumsaini kiungo wa Psg , Manuel Ugarte huku kukiwa na madai pia  ya kumchukua beki wa Bayern Munich na raia wa Uholanzi Matthijs De Ligt.