Victor Osimhen afunguka kwa nini alizikataa Chelsea, PSG na Al Ahli na kujiunga na Galatasaray

Mchezaji huyo aliyetemwa nje ya kikosi cha Napoli aliona dili kadhaa zikifeli kuifanikisha uhamisho wake kuenda PSG, Chelsea na hata Al Ahli ya Saudi Arabia.

Muhtasari

• "Nilikuwa tayari nikiifuata Gala tangu Dries Mertens alipojiunga nao, siwezi kusubiri sasa kuanza nao."

• Baada ya kukamilisha kuhamia klabu hiyo Jumatano, Osimhen alienda kwenye mitandao ya kijamii kueleza furaha yake.

VICTOR OSIMHEN
VICTOR OSIMHEN
Image: X

Mshambuliaji wa Nigeria Victor Osimhen amevunja kimya chake baada ya kumalizika kwa zogo lililokuwa limekumba mustakabali wake kwa muda mrefu.

Mchezaji huyo aliyetemwa nje ya kikosi cha Napoli aliona dili kadhaa zikifeli kuifanikisha uhamisho wake kuenda PSG, Chelsea na hata Al Ahli ya Saudi Arabia.

Baada ya dirisha la uhamisho kufungwa Ulaya, Osimhen alipata upenyo wa kujiunga na Galatasaray ya Uturuki na amevunja kimya chake kwa nini hatimaye alihamia Uturuki.

"Niliposikia kuhusu kupendezwa na Galatasaray, ulikuwa uamuzi rahisi kwangu. Nilijua jinsi Galatasaray ilivyokuwa kubwa, jinsi familia inavyohisi. Ina mashabiki wa ajabu," Osimhen alisema kwenye tovuti rasmi ya klabu.

Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 25 pia alifichua kuwa mtani wake, Henry Onyekuru alichangia pakubwa katika uhamisho huo.

"Nilikuwa tayari nikiifuata Gala tangu Dries Mertens alipojiunga nao, siwezi kusubiri sasa kuanza nao."

Baada ya kukamilisha kuhamia klabu hiyo Jumatano, Osimhen alienda kwenye mitandao ya kijamii kueleza furaha yake.

"Nimefurahi sana kuwa sehemu ya familia ya Galatasaray," aliandika kwenye X.

"Siwezi kungoja kutoa yote yangu na kufaidika zaidi na safari hii mpya na kundi la kushangaza na mashabiki. Tayari kuunda kumbukumbu zisizoweza kusahaulika pamoja! Twende.”