Klabu ya Manchester City imekamilisha
usajili wa mshambuliaji wa Misri Omar Marmoush kutoka klabu ya Eintracht
Frankfurt ya Bundesliga.
Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 25 amekubali kandarasi hadi Juni 2029, baada ya kukamilisha uhamisho wa thamani ya £59m na nyongeza kupanda hadi £4m.
Mchezaji huyo wa kimataifa wa Misri mwenye umri wa miaka 25 ametesa katika Bundesliga na UEFA Europa League, akifunga mara 20 na kuchangia pasi za mabao 13 katika mashindano yote tayari msimu huu.
Kiwango cha Marmoush kimeamsha hisia za Man City, ambao wamekimbia kumfanya kuwa mchezaji wao wa tatu wa usajili wa dirisha la Januari.
Atavaa shati nambari 7.
"Manchester City ni moja ya klabu kubwa duniani katika kipindi cha miaka 10 iliyopita, hivyo halikuwa swali," Marmoush alisema baada ya kukamilisha usajili.
"Ni furaha na heshima kwangu na familia yangu kuiwakilisha Manchester City. Inawafurahisha; inanifurahisha kuwa ndoto zangu zinatimia. Misimu miwili iliyopita imekuwa nzuri, lakini ni mwanzo tu kwa mimi,” aliongeza.
Man City imekuwa imepungukiwa na washambulizi w tangu kuondoka kwa Julian Alvarez majira ya joto yaliyopita. Mchezaji huyo wa kimataifa wa Argentina aliuzwa kwa Atletico Madrid, huku Man City wakiamua kuimarisha nafasi nyingine badala ya kuchukua nafasi yake.
Mabingwa hao watetezi wa EPL pia
wamemsajili mlinzi wa Brazil Vitor Reis mwenye umri wa miaka 19 kutoka Palmeiras
kwa £30m na beki wa Uzbekistan Abdukodir Khusanov kutoka Lens kwa £34m katika
dirisha la uhamisho la Januari.
Marmoush alianza taaluma yake ya soka akiwa na Wadi Degla kwenye Ligi Kuu ya Misri, kabla ya kusajiliwa na VfL Wolfsburg mnamo 2020.
Alicheza kwa mkopo FC St Pauli na VfB Stuttgart kabla ya kuhamia Frankfurt 2023, ambapo alifunga mabao 37 na kutengeneza 20 za mabao katika michezo 67.