
Klabu ya Arsenal imepigwa faini ya pauni 65,000 (Sh10.6m) na Tume Huru ya Udhibiti kufuatia tukio la utovu wa nidhamu wa wachezaji wake wakati wa mechi ya Ligi Kuu ya England dhidi ya Wolverhampton Wanderers mnamo Januari 25.
Kwa mujibu wa tume hiyo, Arsenal ilishindwa kudhibiti wachezaji wake ambao walionyesha tabia isiyofaa katika dakika ya 43 ya mchezo huo.
Klabu hiyo baadaye ilikiri mashtaka hayo, na baada ya kusikilizwa kwa kesi, adhabu hiyo ikawekwa rasmi.
Tukio hilo lilitokea baada ya uamuzi wa mwamuzi ambao haukuwapendeza wachezaji wa Arsenal, na baadhi yao walionekana kumzingira mwamuzi kwa malalamiko makali.Hii ni mara nyingine Arsenal inakumbwa na matatizo ya kinidhamu msimu huu, huku FA ikiwa macho kuhusu mienendo ya wachezaji wa klabu mbalimbali.
Kwa mujibu wa sheria za FA, klabu zinatakiwa kuhakikisha kuwa wachezaji wao wanaheshimu maamuzi ya waamuzi na wanadhibitiwa ipasavyo wakati wa mechi. Kutotii kanuni hizo kunaweza kupelekea adhabu kama hii iliyowapata Arsenal.
Hii si mara ya kwanza Arsenal kupigwa faini kwa kosa kama hili. Katika mechi dhidi ya Newcastle mnamo Novemba 2023, Arsenal pia ilitozwa faini kwa kushindwa kudhibiti wachezaji wake waliokuwa wakimlalamikia mwamuzi baada ya bao la ushindi la Newcastle.
Kocha wa Arsenal, Mikel Arteta, amekuwa akitetea wachezaji wake akidai kuwa wanajitahidi kupambana kwa ajili ya ushindi, lakini FA imekuwa kali katika kuhakikisha nidhamu inazingatiwa ndani ya uwanja.
Kwa sasa, Arsenal
italazimika kulipa faini hiyo huku ikijizatiti kuhakikisha haitumbukii tena
katika matatizo ya kinidhamu msimu huu.
Mechi zao zijazo zitakuwa muhimu si tu kwa matokeo bali pia kwa jinsi wachezaji wao wanavyoshughulikia maamuzi ya waamuzi ili kuepuka adhabu zaidi.