logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Edu amaliza rasmi ukurasa wa Arsenal, amtakia heri mrithi wake

Edu alielezea jinsi alivyopewa jukumu la kuhakikisha Arsenal inarejea katika hadhi yake ya zamani ya ushindani na mafanikio.

image
na Samuel Mainajournalist

Football11 April 2025 - 14:37

Muhtasari


  • Edu ametoa ujumbe wa kuaga rasmi klabu hiyo, akifunga ukurasa wa miaka mitano na nusu ya kujivunia katika historia yake ya taaluma ya soka.
  • Edu pia alituma salamu za heri kwa mrithi wake, Andrea Berta, ambaye ameteuliwa rasmi kuchukua nafasi hiyo nyeti ya michezo.

Edu Gaspar

Aliyekuwa Mkurugenzi wa Michezo wa Arsenal, Edu Gaspar, ametoa ujumbe wa kuaga rasmi klabu hiyo, akifunga ukurasa wa miaka mitano na nusu ya kujivunia katika historia yake ya taaluma ya soka.

Edu, ambaye alijiunga na Arsenal mwezi Julai mwaka 2019 kama Mkurugenzi wa Kiufundi, alihitimisha rasmi kandarasi yake jana, Aprili 11, 2025, baada ya kuwa likizoni tangu Novemba 2024 alipoondoka rasmi kazini.

Katika taarifa aliyotoa Alhamisi kupitia mitandao ya kijamii, Edu alielezea shukrani zake kwa klabu, wachezaji, mashabiki na kila mmoja aliyeshiriki katika safari yake ya kuijenga upya Arsenal.

"Kwa moyo uliojaa shukrani, leo nafungia rasmi mmoja wa sura muhimu zaidi katika taaluma yangu. Baada ya miaka mitano na nusu, safari yangu kama Mkurugenzi wa Michezo wa Arsenal FC imefikia kikomo," alisema Edu.

Edu alielezea jinsi alivyopewa jukumu la kuhakikisha Arsenal inarejea katika hadhi yake ya zamani ya ushindani na mafanikio, akisisitiza kuwa kufuzu kwa Ligi ya Mabingwa Ulaya kilipaswa kuwa kiwango cha chini kwa klabu ya ukubwa kama Arsenal.

"Nilijiunga na klabu nikiwa na dhamira ya kuirejesha Arsenal miongoni mwa vigogo wa soka, kuleta mabadiliko ya kiutamaduni, kushindania mataji, na kuhakikisha kufuzu kwa Ligi ya Mabingwa linakuwa jambo la kawaida," alisema.

Edu pia alikumbuka kwa fahari jinsi alivyoteuliwa kuwa Mkurugenzi wa Michezo wa kwanza katika historia ya klabu, akisema ilikuwa heshima kubwa kwake.

Hakusahau mchango mkubwa wa mashabiki, akisema walikuwa sehemu muhimu ya mafanikio ya mabadiliko ya Arsenal.

"Kwa mashabiki wetu, asanteni kwa moyo wote! Mlioleta nishati, msisimko, na uhusiano wa kipekee kila mechi. Emirates iligeuka kuwa kama toleo jipya la Highbury!" alisema.

Aliwashukuru wamiliki wa klabu Stan na Josh Kroenke, meneja Mikel Arteta, benchi la ufundi, bodi ya wakurugenzi, wachezaji, na wafanyakazi wote wa klabu kwa ushirikiano na ukarimu alioupata.

"Haikuwa rahisi, lakini kazi yetu ya pamoja na roho ya umoja ilinifanya nijihisi kutosheka kwa miaka yote hii," aliongeza.

Edu pia alituma salamu za heri kwa mrithi wake, Andrea Berta, ambaye ameteuliwa rasmi kuchukua nafasi hiyo nyeti ya michezo katika klabu hiyo ya London.

"Ninaondoka nikiwa na moyo wa amani na fahari kubwa kwa kile tulichokijenga pamoja. Nawatakia kila la heri Arsenal FC!"

Edu alisisitiza kuwa alisubiri hadi siku ya mwisho rasmi ya mkataba wake ili kutoa taarifa hiyo, akiheshimu klabu na watu wote waliohusika.

Makala Zinazohusiana


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved