logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Champions League: Ratiba ya nusu fainali ya yathibitishwa baada ya Arsenal kuwaangusha miamba Real Madrid

Mechi za mkondo wa kwanza zitachezwa Aprili 29 na Aprili 30, huku mikondo ya marudiano ikichezwa Mei 6 na Mei 7.

image
na Samuel Mainajournalist

Football17 April 2025 - 07:47

Muhtasari


  • Ushindi huo si tu umerejesha Gunners katika hatua ya juu ya michuano ya bara Ulaya, bali pia umeandaa pambano la kusisimua dhidi ya PSG.
  • Fainali ya Klabu Bingwa Ulaya msimu huu itapigwa Mei 31 katika uwanja wa Allianz Arena mjini Munich.

Gabriel Martinelli alifunga bao lililozima ndoto za Real Madrid

Arsenal walithibitisha rasmi nafasi yao katika hatua ya nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya baada ya ushindi mkubwa dhidi ya mabingwa watetezi Real Madrid mnamo Jumatano usiku.

Ushindi huo si tu umerejesha Gunners katika hatua ya juu ya michuano ya bara Ulaya, bali pia umeandaa pambano la kusisimua dhidi ya Paris Saint-Germain.

Kikosi cha Mikel Arteta kiliduwaza miamba ya Uhispania kwa kuichapa Real Madrid mabao 3-0 katika mechi ya kwanza iliyopigwa Emirates, kabla ya kukamilisha kazi hiyo kwa ushindi wa 2-1 jijini Madrid.

Bukayo Saka na Gabriel Martinelli walifunga mabao hayo muhimu yaliyopelekea ushindi wa jumla wa 5-1 — matokeo yaliyoweka wazi dhamira ya Arsenal kwenye michuano ya msimu huu.

Arsenal sasa watakutana na PSG kwenye nusu fainali. Timu hiyo ya kocha Luis Enrique imeonyesha ubora mkubwa kwa kuwaondoa vilabu vya England — Liverpool katika raundi ya 16 bora na Aston Villa kwenye robo fainali. Ingawa Arsenal waliwahi kuwashinda PSG 2-0 katika hatua ya makundi msimu huu, Wafaransa hao wameimarika na wana matumaini ya kufika fainali kwa mara ya pili katika historia yao.

Kwa upande mwingine wa droo, Barcelona watachuana na Inter Milan. Barcelona waliitoa Borussia Dortmund kwa jumla ya mabao 5-3 na kwa sasa wanapigiwa upatu kutokana na safu yao kali ya ushambuliaji chini ya kocha mpya Hansi Flick, huku wakilenga kushinda mataji matatu msimu huu.

Inter Milan waliibuka na ushindi dhidi ya Bayern Munich kwenye robo fainali kwa kushinda ugenini kisha kutoka sare nyumbani. Kikosi hicho cha Simone Inzaghi sasa kitapambana na Barcelona — timu waliyoifunga mwaka 2010 walipotwaa taji la Champions League chini ya Jose Mourinho.

Mechi za mkondo wa kwanza za nusu fainali zitachezwa Jumanne, Aprili 29 na Jumatano, Aprili 30, huku mikondo ya marudiano ikichezwa Jumanne, Mei 6 na Jumatano, Mei 7.

Fainali ya Klabu Bingwa Ulaya msimu huu itapigwa Mei 31 katika uwanja wa Allianz Arena mjini Munich — uwanja huo ndio ulioshuhudia Chelsea wakiilaza Bayern Munich kwa mikwaju ya penalti mwaka 2012.

Ratiba ya Nusu Fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya

Mikondo ya Kwanza

  • Jumanne, Aprili 29: Arsenal dhidi ya Paris Saint-Germain
  • Jumatano, Aprili 30: Barcelona dhidi ya Inter Milan

Mikondo ya Marudiano

  • Jumanne, Mei 6: Paris Saint-Germain dhidi ya Arsenal
  • Jumatano, Mei 7: Inter Milan dhidi ya Barcelona


Makala Zinazohusiana


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved