Huzuni yatanda huku strika mahiri akifariki wiki kadhaa baada ya kufanya harusi na CEO wa klabu

Ntuli na CEO wa AmaZulu FC, Bi Zungu walifunga pingu za maisha mnamo Septemba 12, 2023.

Muhtasari

•Ntule alifariki katika Midlands Medical Center alipokuwa akitibiwa baada ya kugundulika kuwa na aina kali ya saratani hivi majuzi.

•Miezi miwili iliyopita, Ntuli alifunga ndoa na Ofisa Mtendaji Mkuu wa AmaZulu FC, Sinenjabulo Zungu katika sherehe ya harusi ya kifahari.

Marehemu Bongi Ntule
Image: HISANI

Klabu ya soka ya Afrika Kusini, AmaZulu FC imethibitisha kifo cha nahodha wake,  Bonginkosi Ntuli.

Katika taarifa yake Jumapili jioni, klabu hiyo inayoshiriki Ligi Kuu ya Soka ya Afrika Kusini ilitangaza kuwa mshambuliaji huyo alifariki katika Hospitali ya Kibinafsi ya Midlands Medical Center alipokuwa akipatiwa matibabu baada ya kugundulika kuwa na aina kali ya saratani hivi majuzi.

"Ni kwa moyo mkunjufu kwamba tunawataarifu kuhusu kufariki kwa mshambuliaji wetu mpendwa na mtumishi mwaminifu, Bonginkosi Ntuli," AmaZuluFC ilitangaza Jumapili jioni.

Waliongeza, "Ntuli hivi majuzi aligundulika kuwa na aina kali ya saratani, ambayo ilikithiri na hatimaye kupelekea kifo chake katika Hospitali ya Kibinafsi ya Midlands Medical Center, mjini Pietermaritzburg mchana wa leo (Jumapili)."

Klabu iliitakia roho ya Ntuli mapumziko ya amani na kuwataka watu kuheshimu usiri wa familia, marafiki na watu wa karibu.

"Matangazo zaidi yatatolewa kwa wakati ufaao," ilisema taarifa hiyo.

Maelfu ya mashabiki na vilabu vya soka kote duniani wameungana na klabu ya AmaZulu FC na familia ya Ntuli kuomboleza kifo cha mshambuliaji huyo mwenye umri wa miaka 32.

Kabla ya msimu mpya kuanza, takriban miezi miwili iliyopita, Bongi Ntuli alifunga ndoa na Ofisa Mtendaji Mkuu wa AmaZulu FC, Sinenjabulo Zungu katika sherehe ya harusi ya kifahari iliyofanyika KwaZulu-Natal Midlands. Wawili hao hapo awali walikuwa wamepitia taratibu za ndoa za kitamaduni mwezi Mei 2023 kabla ya kufunga pingu za maisha mnamo Septemba 12, 2023.

Baba mkwe wa Ntuli, babake Zungu ndiye mmiliki wa klabu ya AmaZulu Football ambapo mshambuliaji huyo mwenye kipaji ametumia miaka mitano iliyopita kabla ya kukata roho. Roho yake ipumzike kwa amani.