logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Okutoyi kujiunga na chuo kikuu cha Auburn Marekani

Okutoyi, 18, ni mhitimu wa shule za msingi za Loreto Convent na Mbagathi jijini Nairobi.

image
na

Yanayojiri11 October 2022 - 13:17

Muhtasari


•Anatazamiwa kujiunga na Auburn mnamo Januari 2023.

•Okutoyi alifungua ukurasa mpya katika historia kwa kuwa Mkenya wa kwanza kutawazwa bingwa katika hafla ya Grand Slam.

Angella Okutoyi

Mchezaji mahiri wa tenisi nchini Kenya, Angella Okutoyi, hatimaye amechagua chuo atakachojiunga nacho katika azma yake ya kuwa bingwa wa dunia.

Katika chapisho kwenye ukurasa wake wa mtandao wa kijamii, Okutoyi alifichua kuwa atajiunga na Chuo Kikuu cha Auburn nchini Marekani.

"Nina furaha sana kutangaza kwamba nitaendelea na kazi yangu ya tenisi na masomo katika Chuo Kikuu cha Auburn! Shukrani kwa familia yangu, makocha, marafiki na kila mtu ambaye alinisaidia kufika hapa!" Okutoyi aliandika.

Okutoyi, 18, ni mhitimu wa shule za msingi za Loreto Convent na Mbagathi jijini Nairobi. Pia alihudhuria kituo cha Shirikisho la Tenisi la Kimataifa (ITF) nchini Burundi.

Anatazamiwa kujiunga na Auburn mnamo Januari 2023 baada ya kushiriki mashindano ya W15 Monastir nchini Tunisia mnamo Oktoba 17-23 na W15 Nairobi katika Klabu ya Karen Country jijini Nairobi mnamo Novemba 14-20.

Mnamo Septemba 6, alibanduliwa nje ya mashindano ya wasichana ya US Open baada ya kupoteza kwa Taylah Preston wa Australia.

Okutoyi alikuwa na matumaini ya kufika robofainali, hatua moja kutoka kwa juhudi zake za awali nchini Australia, ambapo alijitoa katika raundi ya tatu.

Okutoyi aliungana na mchezaji wa Uholanzi Rose Marie Nijkamp kushinda taji la Wimbledon Doubles mnamo Juni 20.

Wachezaji hao wawili waliokutana kwenye Instagram, waliwashinda Wakanada Kayla Cross na Victoria Mboko katika fainali ya michuano ya Wimbledon Open doubles Junior Championships katika All England Lawn.

Kisha mnamo Septemba 3, Okutoyi alishirikiana na Malwina Rowinska wa Poland kushinda J1 Repentigny Doubles katika Hifadhi ya Larochelle nchini Kanada.

Okutoyi alifungua ukurasa mpya katika historia kwa kuwa Mkenya wa kwanza kutawazwa bingwa katika hafla ya Grand Slam.


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved