Gavana Tunai ajiunga na UDA kuania useneta wa Narok

Muhtasari

• Naibu rais alipongeza hatua hiyo ya Tunai, huku akionyesha imani yake ya kunyakua urais mwezi Agosti. 

• Tunai katika azma yake ya useneta atachuana vikali na Seneta wa sasa Ledama Ole Kina, Salaton Tompo, Mbunge wa Kilgoris Gideon Konchellah na wengine wengi.

Gavana Samuel Tunai apokelewa kwenye chama cha UDA na Naibu Rais William Ruto. Picha: TWITTER/WILLIAM RUTO
Gavana Samuel Tunai apokelewa kwenye chama cha UDA na Naibu Rais William Ruto. Picha: TWITTER/WILLIAM RUTO

Gavana wa Kaunti ya Narok Samuel Ole Tunai amejiunga na chama cha United Democratic Alliance (UDA) kabla ya Uchaguzi Mkuu wa Agosti. 

Tunai ambaye awali alikuwa mwanachama wa Jubilee Party, alitoa uamuzi huo siku ya Ijumaa. 

Tunai alipokelewa katika chama hicho na Kinara wa UDA Naibu Rais William Ruto katika makazi yake mtaani Karen. Gavana huyo alisema kuwa hatua yake ilitokana na imani yake kwa uaniaji wa urais wa Ruto na mipango yake kwa nchi.

 "Tunaamini kabisa kuwa wewe ndiye mtu mwafaka kuipeleka nchi hii katika ngazi ya juu zaidi. Ninaamini kabisa ajenda yako kwa nchi hii na watu wa Kenya," Tunai alisema. 

Naibu rais alipongeza hatua hiyo ya Tunai, huku akionyesha imani yake ya kunyakua urais mwezi Agosti. 

Kivumbi kikali kinatarajiwa katika Kinyang'anyiro cha kupata gavana wa Narok kati ya aliyekuwa katibu mwandamizi Patrick Ntutu na mbunge wa Narok Kaskazini Moitalel ole Kenta ambaye anawania kwa tikiti ya chama cha ODM. 

Wakati huo huo, Tunai katika azma yake ya useneta atachuana vikali na Seneta wa sasa Ledama Ole Kina, Salaton Tompo, Mbunge wa Kilgoris Gideon Konchellah, mwanaharakati wa haki za ardhi wa Kimasai Meitamei Ololdapash na mchapishaji Andrew ole Sunkuli.