Gavana Waiguru aomba handshake kati ya Uhuru na Ruto

Muhtasari

• Gavana Waiguru amemtaka rais Kenyatta kumaliza tofauti zake na naibu rais William Ruto.

• Alisema kwamba watu wanaomzingira rais hawana nia nzuri.

Gavana wa kaunti ya Kirinyaga, Ann Waiguru sasa anataka kuwepo a hadshake kati ya rais Uhuru Kenyatta na naibu wake William Ruto.

Waiguru alisema kwamba wakazi wa mlima Kenya wanampenda ila hawapendi dharau anazomfanyia naibu wake.

Aidha, alisema kwamba watu wanaomzunguka rais Kenyatta hawana nia nzuri na hivyo kumtaka abadilishe mawazo yake.

"...Angalia wale watu wamekuzunguka, wamekuwa wakikudanganya kwa miaka mingi. Ili ujue wanakudangaya, angalia mahali watu wa mlima Kenya wako na mahali wewe uko," Waiguru alisema.

Alishikilia kwamba wakazi wa mlima Kenya wameshaamua kwamba watamchagua William Ruto kama rais wao katika uchaguzi mkuu ujao.

Alimtaka rais Uhuru Kenyatta kukoma kuzungumza maneno ya uongo kuhusu naibu rais, akisema kwamba wakenya hawawezi kudanganywa.

Alimshauri Kenyatta kufanya mazungumzo na William Ruto na kujiondoa katika siasa ili kutoa mazingira mazuri ya naibu rais kutoana kijasho na Raila Odinga katika kinyang'anyiro cha urais.

Alirejelea kauli ya rais Kenyatta kwamba angehudumu kwa miaka kumi na baadaye amuunge mkono William Ruto katika miaka kumi mingine ya serikali inayofuata.

Waiguru vilevile alisema kwamba kinara wa ODM Raila Odinga ndiye alikuwa na njama ya kupidua serikali ya Kenyatta kwa kitendo chake cha kujiapisha baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2017.

Alimtaka kubadilisha watu wanaomzunguka na kuzingatia kumaliza miradi ya maendeleo katika miezi minne iliyosalia katika hatamu yake.

Kwa sasa inasubiriwa kuona iwapo rais Uhuru Kenyatta atausikia mwito wa gavana huyo na kufanya handshake na naibu rais William Ruto kabla ya Agosti 9.