Kinara wa ODM Raila Odinga ameandaa mkutano wa pamoja na vinara wa vyama tanzu vya muungano wa Azimio La Umoja One Kenya.
Mkutano huo uliofanyika siku ya Alhamisi ulijiri muda mfupi tu baada ya kiongozi wa Maendeleo Chap Chap gavana Alfred Mutua kutishia kuondoka muungano wa Azimio One Kenya kwa kile alitaja kuwa kupuuzwa kwa baadhi ya vyama katika muungano huo.
Mkutano huo ambao madhumuni yake yalikuwa kuzima joto katika muungano wa Azimio ulihudhuriwa na viongozi wa vyama mbali mbali wakiwemo magavana Charity Ngilu wa Kitui (NARC), Dkt. Alfred Mutua wa Machakos (Maendeleo Chap Chap), kinara wa NARC Kenya Martha Karua, Prof. Kivutha Kibwana wa Muungano Party, katibu wa chama cha DAP Kenya Dkt. Eseli Simiyu miongoni mwa wengine wengi.