"Hakuna kitu kama Deep State hapa Kenya, acha uongo!" Matiang'i amjibu Ruto

Muhtasari

• Waziri Matiang'i akizungumza katika mkutano wa kanisa la Kianglikana alipuzilia mbali madai ya kuwepo kwa Deep State.

• Alisema Ruto ndiye amekuwa akidanganya wakenya kuhusu uwezekano wa kitu kama hicho.

Waziri wa usalama Fred Matiang'i na naibu rais William Ruto
Waziri wa usalama Fred Matiang'i na naibu rais William Ruto
Image: Facebook

Waziri wa masuala ya ndani Dkt. Fred Matiang’i ameendeleza kutema cheche za moto dhidi ya naibu rais William Ruto kuhusu maneno ambayo amekuwa akitumia katika kampeni zake, maneno ambayo Matinag’i anasema yanawapotosha Wakenya.

Akizungumza Jumanne katika mkutano wa Maaskofu wakuu wa kanisa la Kianglikana jijini Nairobi, Waziri huyo asiyejua kuweka maneno yake akibani alimjia juu naibu rais na kusema kwamba amekuwa akiwapotosha Wakenya kwa maneno kama Deep State na System, kitu amabcho ni cha kufikirika tu na wala hakipo nchini Kenya.

Viongozi hao wa kanisa walitaka kubaini ukweli wa uwezekano wa Deep State na System nchini Kenya, jambo ambalo Waziri Matiang’i aliwatoa wasiwasi na kutupilia mbali madai hayo ya Ruto na wandani wake.

“Watu ambao wanarindima ngoma za kuwepo kwa Deep State na kunung’unika kwa baraza la usalama wa taifa ndio wale wale wanaoshikilia nyadhifa serikalini na kuwaambia kwamba wana nguvu ya dola na uwezo mkubwa serikalini, sasa hao ni nani? Hizi ni hadithi tu zinasoundwa na kutembezwa tu. Unaendesha pesa katika taifa hilo, unakula chakula kinachonunuliwa na taifa hilo unalonung’unikia, unaishi katika nyumba ya taifa hilo, sasa taifa hilo linakuwaje Deep State?” Matiang’i aliuliza, huku ikionekana anamtupia Ruto maneno haya.

Hii ndio mara ya kwanza Waziri huyo alijibu wazi madai hayo ambayo naibu rais amekuwa akiyazungumzia katika kampeni zake kwa takriban miaka mitatu sasa.