Aliyekuwa gavana wa Nairobi Evans Kidero ameidhinishwa kuania kiti cha gavana wa Homa Bay kama mgombea huru.
Kidero ambaye alikuwa ametangaza kuania kiti hicho kwa tiketi ya ODM na hata kulipa ada za uaniaji aligura ODM baada ya chama hicho kumpa tiketi ya moja kwa moja Gladys Wanga.
Alikabidhiwa cheti cha muaniaji huru siku ya Ijumaa na msajili mkuu wa vyama vya kisiasa Ann Nderitu.
Wiki iliopita Kidero alikuwa ameahidi wafuasi wake kuwa atatangaza mwelekeo wake mpya baada ya ODM kumpokeza tiketi ya moja kwa moja Gladys Wanga kuania wadhifa huo.
Kidero katika ujumbe wake muda mfupi baada ya Wanga kupokezwa tiketi hiyo alisema kwamba watu wa Homa Bay kwa mara nyingine tena wamenyimwa fursa ya kuchagua mgombeaji wa Chama cha ODM wanayempendelea kwa kiti cha ugavana kwa uchaguzi mkuu wa Agosti 9 2022.
“Hili ni jambo la kusikitisha kwa sababu Homa Bay ililipia gharama wakati Dkt. Odhiambo Mbai, ambaye alikuwa mwenyekiti wa Kamati ya Ugatuzi katika Kamati ya Kitaifa ya Marekebisho ya Katiba ya Bomas, alipouawa na wale waliopinga mabadiliko ya Katiba. Tunastahili bora zaidi,” Kidero alisema.
Kidero aliongeza kuwa, “Kama mwana na mpiga kura aliyesajiliwa katika Kaunti ya Homa Bay nitafuata njia mbadala ili kuwapa wapiga kura fursa nyingine ya kumchagua kiongozi wanayemtaka mnamo Agosti 9, 2022.”
Kidero alikuwa amesema kuwa lengo lake kuania ugavana wa Homa Bay lilikuwa kuona Kaunti hiyo ikiimarika kutoka hadhi yake ya sasa hadi kufikia kiwango ambacho wakazi wanaweza kufurahia matunda ya ugatuzi.