"Mimi siogopi hata kama Raila atashindwa na Ruto kuwa rais" - Dkt Matiang'i

Muhtasari

• Waziri wa usalama wa ndani Dkt Fred Matiang'i alisema hana wasiwasi wowote wa kuadhibiwa na William Ruto iwapo ataibuka mshindi wa urais Agosti 9.

Waziri wa usalama Fred Matiang'i na naibu rais William Ruto
Waziri wa usalama Fred Matiang'i na naibu rais William Ruto
Image: Facebook

Waziri wa usalama wa ndani Dkt. Fred Matinag’i anasema kwamba kamwe hatojutia maamuzi yake ya kumpigia debe kinara wa ODM Raila Odinga kuelekea uchaguzi mkuu wa Agosti 9 na kusema kwamba hata kama Raila atashindwa na hasidi wake mkuu William Ruto kushinda kama rais, basi yeye hana wasiwasi wowote wa kuadhibiwa kwa njia yoyote ile na uongozi wa Ruto.

Katika maahojiano ya kipekee na gazeti moja la humu nchini, Matiang’i alisema kwamba yeye hana wasiwasi wowote wa kuhofia maisha yake endapo Ruto atashinda uchaguzi huo kwani uongozi wa rais wa sasa Uhuru Kenyatta si wa kiimla ambao unaweza msababishia wasiwasi wa kuadhibiwa pindi atakapomaliza kuhudumu kama Waziri wa usalama wa ndani.

“Sisi sio jeshi la kiimla ambalo liko madarakani kwa uhalifu kwamba serikali itakayochaguliwa kidemokrasia ikiingia, tutakabiliwa na makosa yetu. Hatutawali kwa uhalifu," alisema Matiang’i.

Waziri huyo ambaye kwa mara kadhaa wametofautiana vikali na naibu rais William Ruto alisema kwamba maisha yataendelea kama kawaida na kusema kwamba uamuzi wake wa kumpigia Raila debe si jambo la kuogopa kwani yeye pia ni mwanadamu na ana kila haki ya kidemokrasia ya kumpigia debe mwaniaji yeyote anayempendelea.

Matiang’i alisema kwamba kwa sasa hana wasiwasi wowote na uongozi utakaokuja, uwe ni ule anaoupigia debe au ule anaoupinga kwani lengo lake kuu kwa sasa ni kuhakikisha nchi haitumbukii katika machafuko ya kivita baada ya uchaguzi kwa kuhakikisha kwamba usalama unadumishwa vilivyo.