Raila Odinga kutangaza mgombea mwenza wake leo kuanzia saa tano asubuhi

Muhtasari

•Raila Odinga alisema atamtaja mtu ambaye atakuwa debeni naye katika Uchaguzi Mkuu wa Agosti 9 katika KICC kuanzia saa tano asubuhi.

•Kuna ripoti kwamba Jopo la kuteua mgombea mwenza wa  Azimio liliafikia kuwa kiongozi wa Narc Kenya Martha Karua ndiye anayefaa zaidi kwa nafasi hiyo.

Kinara wa ODM Raila Odinga na kiongozi wa NARC-K Martha Karua
Kinara wa ODM Raila Odinga na kiongozi wa NARC-K Martha Karua
Image: TWITTER// RAILA ODINGA

Muungano wa Azimio la Umoja- One Kenya unaoongozwa na aliyekuwa waziri mkuu Raila Odinga unatazamiwa kutangaza atakayechukua nafasi ya pili ya uongozi hivi leo.

Akizungumza katika uwanja wa Kamukunji Jumapili, mgombea urais kwa tikiti ya muungano huo Raila Odinga alisema atamtaja mtu ambaye atakuwa debeni naye katika Uchaguzi Mkuu wa Agosti 9 katika KICC kuanzia saa tano asubuhi.

"Nimeangalia hali ya anga na nataka kuwaambia kesho saa tano kule KICC nitatangaza," Raila alisema.

Kiongozi huyo wa ODM amekuwa akipokea shinikizo kubwa kutoka kwa wananchi na viongozi wengine katika muungano huo kutaja mgombea mwenza wake .

Raila alitarajiwa kutangaza mgombea mwenza katika mkutano wa Kamukunji lakini taarifa nyingine kutoka kwa timu yake ikasema ameahirisha hadi Jumatatu.

"Timu yetu inafahamu kuwa Wakenya wana shauku ya kujua mgombea mwenza wa Urais wa Azimio la Umoja One Kenya. Tutatoa tangazo hilo kesho (Jumatatu)," msemaji wa Azimio Makau Mutua alisema.

Kuna ripoti kwamba Jopo la kuteua mgombea mwenza wa  Azimio liliafikia kuwa kiongozi wa Narc Kenya Martha Karua ndiye anayefaa zaidi kwa nafasi hiyo.

Wiki jana, Jopo hilo pia liliwahoji magavana Charity Ngilu (Kitui), Hassan Joho (Mombasa), Lee Kinyanjui (Nakuru) na Wycliffe Oparanya (Kakamega) na kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka kuwania nafasi ya mgombea mwenza .

Wengine ni pamoja na Mwakilishi wa Wanawake wa Murang'a Sabina Chege, Waziri wa Kilimo Peter Munya na aliyekuwa Mbunge wa Emgwen Stephen Tarus.