Raila amteua kakake Kindiki Kithure kuwa mmoja wa maajenti wake wakuu

Muhtasari

•Kithure na Isaiah ambao wote ni maprofesa  ni ndugu wanaounga mkono pande mbili tofauti za kisiasa.

•Raila na mgombea mwenza wake Martha Karua waliidhinishwa kuwania urais katika uchaguzi wa mwaka huu siku ya Jumapili.

Wafuasi wa Azimio la Umoja wakati wa mkutano wa kampeni wa Raila Odinga huko Kilgoris Kaunti ya Narok Jumamosi, Mei 21,2022.
Wafuasi wa Azimio la Umoja wakati wa mkutano wa kampeni wa Raila Odinga huko Kilgoris Kaunti ya Narok Jumamosi, Mei 21,2022.
Image: TWITTER// RAILA ODINGA

Mgombea urais wa Azimio One Kenya Raila Odinga amemteua Saitabao Ole Kanchory kama Ajenti wake Mkuu katika uchaguzi  wa Agosti 9. 

Akizungumza baada ya kupokea cheti cha uteuzi, Raila aliwataja viongozi wengine wanne ambao watakuwa naibu wa Kanchory. 

“Nimemteua wakili Saitabao Kanchory kuwa ajenti mkuu wa kitaifa, naibu wake atakuwa Dkt Carolyne Karugu, Prof Isaiah Kindiki, Dkt Oduor Ong'wen na mshauri wangu wa kisheria Paul Mwangi,” Raila alisema. 

Kithure na Isaiah ambao wote ni maprofesa  ni ndugu wanaounga mkono pande mbili tofauti za kisiasa.

 Siku ya Jumamosi Profesa Kithure aliteuliwa kama ajenti mkuu wa Naibu Rais William Ruto katika uchaguzi wa Agosti. 

Prof Kindiki atasaidiwa na Katibu Mkuu wa United Democratic Alliance Veronica Maina na Gavana wa Turkana Josphat Nanok. 

Prof Kithure ni mshirika wa Ruto wa kisiasa ambaye alikuwa miongoni mwa waliotazamiwa kuwa mgombea mwenza wake, huku kaka yake, Prof Isaiah Kindiki akiwa mfuasi sugu wa Raila.

Maajenti wa Raila watafanya kazi  pamoja na maajenti wa uchaguzi katika uchaguzi wa Agosti. 

Waziri Mkuu huyo wa zamani na mgombea mwenza wake Martha Karua waliidhinishwa kuwania urais katika uchaguzi wa mwaka huu siku ya Jumapili.

Mwenyekiti wa IEBC Wafula Chebukati ambaye ndiye msimamizi wa uchaguzi wa Urais alimtangaza kiongozi wa Azimio kuwa mgombeaji rasmi saa tano kamili asubuhi.

"Stakabadhi ziko sawa na ninaidhinisha uteuzi wa Raila Odinga kama mgombeaji urais katika uchaguzi wa Agosti 9," alisema. 

"Ninawasilisha cheti kwa Raila Odinga kama mgombeaji urais." 

Kiongozi huyo wa ODM aliitaka tume hiyo kuhakikisha uchaguzi huo ni huru, haki na unaweza kuthibitishwa.

MHARIRI: DAVIS OJIAMBO