Natembeya aidhinishwa kuwania ugavana wa Trans Nzoia

Muhtasari
  • Natembeya aliwaomba washindani wake waepuke vurugu, vitisho na matusi wakati wa kampeni
Mratibu wa Bonde la Ufa George Natembeya. Picha: JOSEPH KANGOGO
Mratibu wa Bonde la Ufa George Natembeya. Picha: JOSEPH KANGOGO

Aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Bonde la Ufa George Natembeya aliidhinishwa Jumatatu alasiri na IEBC kuwania ugavana katika uchaguzi wa Agosti.

Afisa Msimamizi wa Uchaguzi katika Kaunti ya Trans Nzoia John Lorionokou aliwaidhinisha Natembeya na mgombea mwenza wake Philomena Bineah Kapkori katika Makavazi ya Kitaifa ya Kenya katika mji wa Kitale.

Natembeya, anayegombea kwa tikiti ya Chama cha Democratic Action of Kenya, aliidhinishwa wakati wa zoezi lililohudhuriwa na Waziri wa Ulinzi Eugene Wamalwa na waziri wa zamani wa baraza la mawaziri Noah Wekesa.

Natembeya aliwaomba washindani wake waepuke vurugu, vitisho na matusi wakati wa kampeni.

Msimamizi huyo wa zamani aliwaambia maelfu ya wakaazi ambao walikuwa wamejitokeza kushuhudia kibali chake watarajie huduma bora na uchumi unaoleta mabadiliko.

"Ninawapa changamoto wapinzani wangu kukumbatia kampeni ya amani. Wanapaswa kuacha vitisho na matusi," alisema.

"Tarajieni uongozi wa kimabadiliko chini ya usimamizi wangu. Ninaahidi sitawaangusha. Timu yetu inaenda kuikomboa kaunti kutoka kwa machafuko ya kiuchumi," aliahidi.

Tume ilikataa mapema kumwidhinisha  mgombeaji huru Profesa Ben Wanjala baada ya mgombea mwenza wake kukosa kutoa hati zilizoidhinishwa.

Wawili hao walipewa hadi kesho.

Wagombea wengine ambao wameidhinishwa ni wagombeaji huru Jimmy Nduruchi na Wycliffe Eshiwani.