Tutarudishia kanisa la PCEA-Gachagua asema serikali ya Kenya Kwanza itabatilisha sare za polisi za blue

Muhtasari
  • Gachagua asema serikali ya Kenya Kwanza itabatilisha sare za polisi za blue
Naibu Rais William Ruto akiwa na Mbunge wa Mathira Rigathi Gachagua wakati wa mkutano wa hadhara huko Githunguri, Kiambu Ijumaa, Februari 18, 2022.
Naibu Rais William Ruto akiwa na Mbunge wa Mathira Rigathi Gachagua wakati wa mkutano wa hadhara huko Githunguri, Kiambu Ijumaa, Februari 18, 2022.
Image: Picha: DPPS

Mgombea mwenza wa Naibu Rais William Ruto Rigathi Gachagua amemkashifu Waziri wa Usalama wa Ndani Fred Matiang'i na Katibu Mkuu wake Karanja Kibicho kutokana na kile alichokitaja kama dhuluma dhidi ya maafisa wa polisi.

Akizungumza wakati wa mkutano wa kampeni katika Kaunti ya Nyandarua siku ya Jumamosi, Gachagua alisema iwapo timu ya Kenya Kwanza inayoongozwa na DP Ruto itatwaa mamlaka mnamo Agosti, itarejesha heshima katika huduma ya polisi.

Mbunge wa Mathira aliweka wazi kuwa atabatilisha sare ya polisi na kuirudisha katika kanisa la PCEA ambako ni yake kulingana na yeye.

Pia alidai kuwa maafisa wa polisi wameteseka mikononi mwa Waziri wa Mambo ya Ndani na Katibu Mkuu wake - Fred Matiang'i na Karanja Kibicho - na ana nia ya kumaliza yote.

"Mumesumbuliwa sana na Matiang'i na Kibicho. Ata ile uniform ya blue ambayo hawataki, tutawaondolea tuwarudishie ile ya Kitambo. Hiyo ya blue tutarudishia kanisa ya PCEA. Hiyo ni uniform ya women's guild,"Alisema Gachagua.

Gachagua alishikilia kuwa Kenya Kwanza inafahamishwa kikamilifu kuhusu changamoto zinazokabili huduma ya polisi na akashtumu wizara ya mambo ya ndani kwa kuwatelekeza wanaume hao waliovalia sare.

Pia aliwakashifu Matiang’i na Kibicho ambao aliwashutumu kwa kuwatisha maafisa wa polisi na maafisa wengine wa serikali kumuunga mkono mgombeaji wa Azimio la Umoja, Raila Odinga.

"Tunataka kuambia machiefs,tumesikia vile munatishwa ati msaidie Raila kushinda kura ati msipomsaidia mtafutwa. Msijali, imebaki siku 57 tutarudisha nyinyi kwa kazi. Tunataka kuwahakikishia maafisa wote kuwa kazi zao hazitapotea."