Mbunge Sankok afunguka sababu za kujiondoa kwenye siasa

Muhtasari

•Sankok alisema nahitaji muda kuangazia biashara zake na ndio maana jina lake halitakuwa kwenye debe.

•Alisema kuwa alianza kutetea watu wanaoishi na ulemavu akiwa umri mdogo sana, na hakupata wakati wa kujijenga.

MBUNNGE MTEULE SANKOK
Image: RADIOJAMBO

Mbunge maalum David Sankok ameeleza ni kwa nini hatawania wadhifa wowote katika uchaguzi wa Agosti.

Kulingana na Sankok, anahitaji muda kuangazia biashara zake na ndio maana jina lake halitakuwa kwenye debe.

"Suala la kugombea au kutogombea ni uamuzi wa kibinafsi. Niliamua safari hii kutotafuta nafasi yoyote ya kuchaguliwa, nahitaji kufanya biashara yangu kidogo," alisema katika mahojiano na kituo kimoja cha redio cha hapa nchini Jumatatu.

Alisema kuwa alianza kutetea watu wanaoishi na ulemavu akiwa umri mdogo sana, na hakupata wakati wa kujijenga.

"Kwa sababu nilianza kujihusisha na utetezi wa watu wanaoishi na ulemavu nikiwa na umri mdogo sana. Kwa hiyo sikupata muda wa kujiendeleza."

Sankok, hata hivyo, alisisitiza kuwa licha ya kutotafuta nafasi ya kuchaguliwa, ataendelea kupigia debe masuala yanayohusu watu wenye ulemavu ambayo anayathamini.

Katika mahojiano hayo, mbunge huyo aliyeteuliwa pia alifafanua kuhusu mpango wa Kenya Kwanza kwa watu wanaoishi na ulemavu nchini.

Pia alitetea muda wake Bungeni akisema ameshiriki kikamilifu katika mijadala inayogusa masuala ya kitaifa, pamoja na masuala yanayowagusa watu wenye ulemavu nchini.

Hii, alisema ilimwezesha kupigiwa kura kuwa mbunge bora wa kiume na wa pili kwa jumla kwa miaka mitatu.

"Siku zote ninafika kwa wakati kwa sababu sitaki chochote kipite bila mimi kuzungumzia suala la watu wenye ulemavu. Nilitambuliwa kama mbunge wa kiume aliyefanya vyema kwa miaka mitatu," Sankok alibainisha.

Hapo awali aliwahi kusema kuwa kuteuliwa katika Bunge la Kitaifa kumeathiri pakubwa kifedha.