• Sankok alisema kwamba huenda alinukuliwa vibaya na watu.
• Amesema hawezi staafu siasa na miaka 43 hali ya kuwa wapo watu wenye miaka 80 kwenye siasa.
Mbunge mteule David Ole Sankok kwa mara nyingine amezidi kuchanganya wakenya wasijue kama yupo kwenye siasa ama amestaafu kama ambavyo ilisemekana mapema wiki hii.
Jumatatu akiwa katika mahojiano ya kipekee na kituo kimoja cha redio humu nchini, Sankok alisema kwamba jina lake halitakuwa katika debe katika uchaguzi mkuu wa Agosti 9.
Wengi wa wafuasi wake walichukulia taarifa hiyo kwamba Sankok ameamua kustaafu kutoka tasnia ya siasa na kuanza shughuli zingine tofauti.
Sasa mbunge huyo mteule anayewakilisha watu wenye ulemavu katika bunge ameweka wazi kwamba hakusema anastaafu kama ambavyo baadhi ya watu wamekuwa wakisema tangu Jumatatu.
Sankok alisema kwamab huenda alinukuliwa vibaya na kunyoosha rekodi ambapo alisema hana mpango wa kustaafu kutoka siasa kwani yeye bado ni mdogo na kusema kwamba ni likizo ndefu tu aliamua kuchukua ili kujitathmini, haswa baada ya kumpoteza mwanawe.
“Sijasema kuwa nastaafu siasa, nilisema siendi kugombea kiti cha kuchaguliwa sawa na Prof Kindiki na Sabina Chege. Tuna watu wenye umri wa miaka 80 kwenye siasa, je naonekana naweza kuacha siasa nikiwa na miaka 43?” Sankok aliweka wazi katika mahojiano na kituo kimoja cha runinga Jumanne asubuhi.
Mbunge huyo aidha alisisitiza kwamba yeye yupo nyuma ya naibu rais William Kwanza na mrengo wa UDA licha ya kujiondoa kwenye siasa kwa muda.
Familia ya Sankok wiki kadhaa zilizopita ilijipata katika wakati mgumu wa majonzi na simanzi baada ya mwanawe aliyekuwa akisoma shule ya upili kujifyatulia risasi na kujiua katika chumba kimoja nyumbani kwao kwenye kaunti ya Narok.
Baadhi wanahisi mshtuko wa kumpoteza mwanawe kwa mtutu wa bunduki aliojielekezea ndilo jambo limemtikiza Sankok mpaka kufikia uamuzi wa kucvhukua likizo ndefu kutokana na masuala ya kisiasa ili kujitathmini upya, haswa baada ya kifo cha mwanawe kutumiwa na baadhi ya watu kuendesha siasa za kuapizana.