(Video) Babu Owino na mpinzani wake Francis Mureithi waweka tofauti kando na kuhubiri amani

Babu Owino wa ODM na Francis Mureithi wa UDA wamekuwa wakimenyanya katika uchaguzi wa Embakasi Mashariki tangu 2017.

Muhtasari

• Babu Owino pia alifichua yeye na Mureithi ni marafiki wakubwa na huwa wanaongea tangu mwaka wa 2016 wakianza kampeni za Embakasi Mashariki.

• Alisema hata kabla ya tukio la Jacaranda, Mureithi alimpigia simu saa mbili usiku wakazungumza zaidi ya saa moja.

Mbunge wa Embakasi ya mashariki Babu Owino Jumatano alishiriki hafla ya maombi ya amani ambayo waliandaa na yeye kwa ushirikiano wa mpinzani wake mkuu katikakinyang’anyiro cha ubunge huko, Francis Mureithi.

Kupitia ukurasa wake wa Facebook, Babu Owino alipakia picha kadhaa na video wakikumbatiana kwa furaha ya undugu na Mureithi ambaye wamekuwa wakioneshana kivumbi katika majukwaa mbali mbali ya kunadi sera kwa wapiga kura ili kuchaguliwa kama mbunge katika uchaguzi mkuu wa Agosti 9.

Hafla hiyo ilikaribisha watu wa haiba mbali mbali wakiwemo maafisa wa polisi, waratibu wa usalama katika eneo hilo, wahubiri pamoja na wafuasi wa pande zote mbili.

“Mimi sina chuki, mbele ya mwenyezi Mungu na Francis Mureithi, mbele ya mwenyezi Mungu na ninaelekeza kidole change juu, kama mimi ndio nilipanga vuruga dhidi ya Mureithi na Ruto, Mungu anifanyie chochote anataka,” alisema Owino.

Babu Owino alimtaka Francis Mureithi kupoteza chuki zote na kusalimiana mbele ya watumishi wa Mungu, na pia kufichua kwamba amani ni ya muhimu kwani wafuasi wao hawafai kupigana na kuchukiana kwa sababu wao wenyewe hupigiana simu na kuzungumza kwa saa kadhaa licha ya kuoneshana nje kwamba wana uhasama.

Wiki chache zilizopita palishuhudiwa vuta nikuvute baina ya mirengo miwili ya Azimio na Kenya Kwanza katika uwanja wa Jacaranda, vurugu ambazo zilisababisha majeraha kidogo kwa Mureithi.

Owino ambaye ni mbunge wa sasa analenga kukiifdhi kiti hicho kupitia tikiti ya chama cha ODM, huku mpinzani wake mkubwa, Mureithi akilenga kumng’oa kwa kutumia chama cha naibu rais, UDA.

Mnamo 2017, wawili hao walimenyama katika kinyang’anyiro ambacho kilishuhudia upinzani mkali ambapo Owino aliibuka mshindi, akimshinda Mureithi kwa kura chache sana, jambo lililopelekea Mureithi kupeleka kesi mahakamani, kesi ambayo baadaye ilidumisha ushindi wa Owino.

Katika uchaguzi mkuu ujao wa Agosti 9, eneo bunge la Embakasi Mashariki tena linatajwa kuwa miononi mwa sehemu ambazo zitashuhudia ushindani mkali huku baadhi ya tafiti zikionesha wawili hao bado wamekaribiana sana katika umaarufu.