(Video) Raila: Kura ya maoni inaonesha Ruto amenishinda Bungoma, aibu kwenu wana Bungoma!

Raila alisema watu wa Bungoma wamemkasirisha kwa kumpendelea Ruto kwenye kura za maoni.

Muhtasari

• Raila alidokeza kwamab haan furaha kwa sababu anaona kama watu wa Bungoma wanamsaliti pamoja na mababu zao wa kisiasa.

Kinara na mpeperusha bendera wa muungano wa Azimio la Umoja One Kenya, Raila Odinga amewasuta vikali watu wa kaunti ya Bungoma kwa kile alisema kwamba ni aibu kumpendelea naibu wa rais ambaye pia ni kinara wa vuguvugu la Kenya Kwanza, William Ruto katika kinyang’anyiro cha urais na kumtenga yeye.

Raila akizungumza katika mkutano wa kisiasa eneo la Kimilili siku ya Ijumaa, aligusia historia jinsi muungano wao uliwajumuisha watu wa kutoka eneo hilo miaka ya 90 kupigania uhuru na demokrasia ya vyama vingi dhidi ya serikali dhalimu ya rais hayati Daniel Moi.

Alisema kwamba matokeo ya kura ya maoni yaliyofanyika wiki jana katika kaunti ya Bungoma yalimuonesha William Ruto akiwa mbele kwa karibia asilimia 60 huku Raila akimfuata kwa umbali wa asilimia 40, jambo ambalo Raila aliwalaumu wakaazi wa kaunti hiyo na kusema ni aibu kwamba wanakubali Ruto ambaye alikuwa anapiga demokrasia ya vyama vingi miaka ya tisini.

“Kura ya maoni yenye ilifanyika wiki jana inaonesha kwamab Ruto anaongoza kwa 60% na Raila anafuata kwa 40% katika kaunti ya Bungoma. Aibu kwenu nyinyi watu. Aibu kwenu! Nahisi kuchukizwa kwa sababu hawa ni watu wangu. Naangalia jinsi watu kutoka huku tuling’ang’ana nao kuleta ukombozi wa pili, nafikiria Masinde Muliro, nafikiria Kijana Wamalwa,” Raila alisema kwa hasira huku akiwataka wale wote walioko upande wa Ruto kujiunga na muungano wake ili kumpigia kura katika uchaguzi mkuu wa Agosti 9.

Ikumbukwe kaunti ya Bungoma ndio kaunti ya nyumbani ya seneta Moses Wetangula ambaye anampigia naibu rais William Ruto debe kuelekea uchaguzi mkuu baada ya kutofautiana na Raila Odinga kisiasa.

Ruto aliwataka Wetangula na Mudavadi ambao wote wanatoka eneo la Magharibi kuhakikisha kwamba wanamzolea asilimia 70 ya kura zote za mkoa huo ili kujipatia nafasi murwa ya kupata vyeo na mamlaka kwa asilimia 30 katika serikali yake iwapo atashinda kama rais katika uchaguzi huu unaotarajiwa takribani wiki mbili zijazo.