Uhuru alikataa ushauri wangu kuhusu kandarasi za Uchina - Ruto

Ruto alidai kuwa wakati mwingi alijaribu kumshauri rais lakini ushauri wake haukutiliwa maanani

Muhtasari

• Naibu Rais Ruto alijiondolea lawama akidai kuwa nafasi yake ni ya kumuunga mkono rais, akisema kwamba hana usemi wa mwisho.

Naibu Rais William Ruto
Naibu Rais William Ruto

Naibu rais William Ruto amefichua kwamba alikuwa akimshauri rais Uhuru Kenyatta kuweka wazi kandarasi zote ambazo serikali imetia saini na nchi na mashirika ya kimataifa.

Naibu rais ambaye alikuwa akizungumza wakati wa mdahalo wa urais siku ya Jumanne katika Chuo Kikuu cha CUEA alisema kwamba mara nyingi alimtaka rais Kenyatta kukakisha kwamba kandarasi zote za serikali zinapaswa kuwekwa wazi kwa umma ili wananchi wajuwe.

Ruto alikuwa na wakati mgumu kujitenga na maovu ya serikali ya Jubilee huku upande mwingine akijihusisha na mafanikio ya serikali hiyo.

Ruto alidai kuwa wakati mwingi alijaribu kumshauri rais lakini ushauri wake haukutiliwa maanani, alimnyoshea kidole Rais Uhuru Kenyatta kwa kushindwa kuchapisha kandarasi za serikali ya Kenya na ile ya Uchina.

Naibu Rais Ruto alijiondolea lawama akidai kuwa nafasi yake ni ya kumuunga mkono rais, akisema kwamba hana usemi wa mwisho.

Kulingana na DP, majukumu yake yanajumuisha kutumikia watu wa Kenya, kutekeleza majukumu yoyote aliyopewa na sheria na kumshauri rais wakati wowote anapohitajika kufanya hivyo.

“Kama DP kuna mengi unaweza kufanya, nimetekeleza majukumu hayo kwa uwezo wangu wote na nimeweka wazi msimamo wangu kuhusiana na mikataba ya ofisi zinazofaa, si jambo ambalo ningetaka kulitoa kwa umma kwa madhumuni ya kuhakikisha kuwa serikali inafanya kazi,” alisema.

“Nimetoa ushauri kwa mkubwa wangu katika masuala mengi likiwemo suala hilo, nimeeleza vizuri kwamba ni msimamo wa kikatiba kwamba kila mkataba unawekwa hadharani, ushauri huo nimeutoa kwa rais kama inavyotakiwa kwangu lakini unajua mamlaka ya mkubwa".