Paul Otuoma anyakua kiti cha ugavana Busia

Otuoma alipata kura 164, 478.

Muhtasari

•Otuoma sasa atachukua mikoba kutoka kwa gavana anayeondoka Sospeter Ojaamong ambaye amekamilisha mihula yake miwili.

Gavana mteule wa Busia Paul Nyongesa Otuoma (kulia), akikabidhiwa cheti cha uteuzi kutoka kwa afisa mkuu wa uchaguzi kaunti ya Busia.
Gavana mteule wa Busia Paul Nyongesa Otuoma (kulia), akikabidhiwa cheti cha uteuzi kutoka kwa afisa mkuu wa uchaguzi kaunti ya Busia.

Mgombea ugavana wa ODM katika kaunti ya Busia Paul Nyongesa Otuoma ameshinda kiti hicho baada ya jaribio la pili.

Matokeo yaliyotangazwa na Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) yalionyesha  kuwa Otuoma alipata kura 164, 478.

Mshindani wake wa karibu John Sakwa Bunyasi, ambaye amekuwa mbunge wa Nambale  alimaliza wa pili kwa kura 92,144. Bunyasi aligombea kwa tiketi ya chama cha ANC chini ya muungano wa Kenya Kwanza.

Otuoma alimteua aliyekuwa mbunge wa Teso Kaskazini Arthur Odera kama naibu wake ili kusawazisha mlingano wa kikabila katika kaunti hiyo iliyo na idadi kubwa ya watu wa jamii ya Waluhya wakifuatwa na jamii ya Wateso miongoni mwa makabila mengine mengi.

Katika hotuba yake fupi punde tu baada ya kupewa cheti na IEBC Otuoma aliahidi kuunganisiha makabila yote katika kaunti hiyo ili kundelea kuishi kwa amani.

Otuoma ambaye ana tajiriba ya usimamizi katika mashirika ya kimataifa aliwahakikishia wananchi wa kaunti hiyo ya mpakani kuwa ataboresha utendakazi wa kaunti kwa manufaa ya wananchi. 

Otuoma sasa atachukua mikoba kutoka kwa gavana anayeondoka Sospeter Ojaamong ambaye amekamilisha mihula yake miwili. 

Wakati huo huo mwanaharakati Okiya Omutata alitangazwa seneta mteule wa Busia, huku Catherine Omanyo akichaguliwa Mwakilishi Mwanamke wa kaunti hiyo.  

MHARIRI: DAVIS OJIAMBO.