Mama Miradi Millicent Omanga akubali matokeo, ampongeza Passaris kwa ushindi

Awali Polycarp Igathe pia alitangaza kukubali matokeo ya kumpongeza mshindi Johnson Sakaj

Muhtasari

• "Esther Passari ameshinda, anastahili usaidizi wetu na maombi anaposimamia ofisi ya mwakilishi wa kike kwa miaka 5 ijayo. Mungu ibariki nchi yetu,” Omanga aliandika.

Seneta mteule Millicent Omanga
Seneta mteule Millicent Omanga
Image: TWITTER//MILLICENTOMANGA

Millicent Omanga, senata mteule amekuwa wa hivi punde kukubali matokeo na kumpongeza mshindani wake aliyeshinda baada ya matokeo kuwekwa wazi rasmi.

Omanga alikuwa anawania uwakilishi wa kina mama katika kaunti ya Nairobi kupitia tikiti ya chama cha UDA dhidi ya mshindani wake Esther Passaris ambaye alikuwa anakitetea kiti hicho kwa tikiti ya chama cha ODM.

Passaris alitangazwa mshindi na msimamizi mkuu wa uchaguzi katika kauti ya Nairobi Albert Gogo baada ya kujizolea kura 698,929 dhidi ya Omanga aliyekuwa karibu kwa kura 586,246.

Kupitia ukurasa wake wa Twitter, Omanga aliwashukuru wafuasi wake kwa kumpiga kura kwa wingi wa zaidi ya nusu milioni na pia kumpongeza Passaris kwa kukitetea kiti chake.

“Ninataka kuwashukuru watu wa Nairobi walionipigia kura na wale ambao hawakunipigia kura. Ninakubali matokeo ingawa hayakuegemea upande wangu. Esther Passari ameshinda, anastahili usaidizi wetu na maombi anaposimamia ofisi ya mwakilishi wa kike kwa miaka 5 ijayo. Mungu ibariki nchi yetu,” Omanga aliandika.

Awali Polycarp Igathe pia alitangaza kukubali matokeo ya kumpongeza mshindi Johnson Sakaja ambaye walikuwa wanamenyana katika kipute cha ugavana wa Nairobi.

Sasa ni wazi kwamba muungano wa Azimio la Umoja One Kenya umejinyakulia viti viwili kati ya vitatu vikuu katika kaunti ya Nairobi baada ya Edwin Sifuna na  Esther Passaris wote kutoka ODM kushinda nyadhifa za Useneta na uwakilishi wa kike mtawalia.