Simba Arati adai kapunguza bajeti ya kuapishwa kutoka Ksh.57M hadi 3.5M

Magavana wapya wa kaunti wataapishwa Alhamisi, Agosti 25.

Muhtasari

•Kuhusiana na kile kilichojumuisha Ksh.57 milioni, Arati alifichua kwamba kamati ya kaunti ya ofisi ya kaunti hiyo ilikuwa imetenga Ksh.33 milioni kwa ununuzi wa gari jipya la Gavana na naibu wake.

Mwaniaji wa ugavana wa Kisii Simba Arati wakati wa kikao na wanahabari katika afisi ya eneo la Azimio mjini Kisumu Jumamosi. Picha: MAURICE ALAL
Mwaniaji wa ugavana wa Kisii Simba Arati wakati wa kikao na wanahabari katika afisi ya eneo la Azimio mjini Kisumu Jumamosi. Picha: MAURICE ALAL
Image: MAURICE ALAL

Huku magavana wateule wa kaunti wakijitayarisha kula kiapo siku ya Alhamisi, Agosti 25, serikali kadhaa za kaunti ziko mbioni kuhakikisha hafla hiyo imefanyika kwa viwango wanavyovitaka. 

Mfano halisi ni Kaunti ya Kisii ambapo imeripotiwa kuwa Kamati ya mpito kwa Afisi ya Gavana ilikuwa imepanga kutumia Ksh.57 milioni kwa ajili ya kumuapisha gavana mteule na naibu wake kabla ya kuchukua usukani.

Jumatano, gavana mteule wa Kisii Simba Arati alidai kuwa amekataa mgao huo na kushauri kwamba upunguzwe hadi Ksh.3.5 milioni.

“Bajeti iliyokuwa imetengwa kwa ajili ya kuchukua ofisi baada ya kuchaguliwa kwangu ilikuwa Ksh.57 milioni. Nimeipunguza hadi Ksh.3.5 milioni. Itakuwa tu ya juu kwa Ksh.600,000 kwa sababu ya matangazo ya TV ambayo tayari walikuwa wameweka na kwa matangazo ya moja kwa moja," Arati alisema.

Aliongeza kwa kusema kuwa “Siwezi kutumia Ksh.57 milioni wakati hospitali na zahanati katika kaunti hazina dawa na wakaazi wa Kisii hawana maji.”

Kuhusiana na kile kilichojumuisha hadi kufikia  Ksh.57 milioni, Arati alifichua kwamba kamati ya kaunti ya ofisi ya kaunti hiyo ilikuwa imetenga Ksh.33 milioni kwa ununuzi wa magari mapya ya gavana na naibu wake.

Arati, alisema kuwa zaidi ya, Ksh.7 milioni na Ksh.6 milioni zilikuwa zimetengwa kwa ajili ya ukarabati na ujenzi wa ofisi na makazi ya Gavana mtawalia,Ksh.10 milioni zilikuwa zimetengwa kwa hafla ya kuapishwa.