Ghost Mulee aadhimisha kifo cha kaka yake mpendwa Mike

Ni takriban mwaka moja tangu Ghost alipompoteza kaka yake Mike.

Muhtasari

•Mike aliaga dunia mwezi Desemba mwaka uliopita baada ya kupambana na ugonjwa wa figo kwa muda.

•Ghost alimtaja marehemu kama rafikiye, shabiki na mshauri wake mkubwa.

Ghost Mulee na marehemu Mike
Image: INSTAGRAM// GHOST MULEE

Ni takriban mwaka mmoja sasa tangu mtangazaji wa kipindi cha Gidi na Ghost asubuhi kwenye Radio Jambo, Jacob 'Ghost' Mulee alipompoteza kaka yake Mike.

Mike aliaga dunia mwezi Desemba mwaka uliopita baada ya kupambana na ugonjwa wa figo kwa muda.

Huku akiadhimisha mwaka mmoja tangu kifo cha kaka yake siku ya Alhamisi, Ghost alimtakia marehemu mapumziko ya amani.

"Ni mwaka tangu uende na Bwana. Endelea kupumzika kwa amani Mike!" alisema kupitia ukurasa wake wa Instagram.

Ghost na kakake Mike walikuwa na uhusiano wa karibu sana. Wawili hao hawakuwa ndugu tu bali pia walikuwa marafiki wakubwa.

Wakati akimuomboleza kaka huyo wake Desemba mwaka jana, Ghost alimtaja kama rafikiye, shabiki na mshauri wake mkubwa.

"Mike ndugu yangu umepigana vita vizuri. Bwana akupe kibali mpaka tukutane tena! Safiri salama ndugu yangu rafiki yangu shabiki wangu mshauri wangu! Mungu anaweza!" mtangazaji huyo mahiri alisema kwenye Instagram.

Mapema mwaka jana, kocha huyo wa zamani wa Harambee Stars aliandamana na Mike hadi nchini India ili kumtolea figo moja baada ya vipimo vya daktari  vilivyofanyika hapa nchini kubaini marehemu alihitaji figo nyingine.

Hata hivyo walipofika India, upasuaji wa kubadilisha figo haukufanyika kwani mtaalamu aliyekuwa akimhudumia marehemu alipata figo yake kuwa sawa na akasema sio lazima.Ghost aliporejea alithitisha kuwa hakutolewa figo.

Mashabiki wa mtangazaji huyo mahiri wameendelea kumtumia jumbe nzuri za kumfariji huku akimkumbuka marehemu kaka yake.