Kawira afunguka kuolewa akiwa bikira, masaibu yaliyomfanya atoroke baada ya miaka 6

Muigizaji huyo alifichua kuwa masaibu katika ndoa yake yalianza mnamo siku ya harusi

Muhtasari

•Kawira alikashifu ndoa yake ya zamani na kufichua kuwa kuna masuala mengi ambayo yalichangia kuondoka kwake.

"Nilifanya harusi ya kanisa. Nilikuwa bikra nikienda kuolewa.  Nilikuwa nimeenda kwake mara mbili tu," alisema.

Muigizaji Joy Karambu almaarufu Kawira
Muigizaji Joy Karambu almaarufu Kawira
Image: HISANI

Aliyekuwa muigizaji wa Papa Shirandula, Joy Karambu, almaarufu Kawira amefunguka kuhusu kuvunjika kwa ndoa yake ya miaka sita.

Katika mahojiano na Massawe Japanni alipotembelea studio za Radio Jambo mnamo Jumatano, Kawira alikashifu ndoa yake ya zamani na kufichua kuwa kuna masuala mengi ambayo yalichangia kuondoka kwake.

"Kuna wakati mwingine huwa unavumilia unaona haifai. Nilivumilia muda mrefu sana," alisema.

Muigizaji huyo alifichua kuwa masaibu katika ndoa yake yalianza mnamo siku ya harusi, Novemba 2, 2014.

Alisema kuna matatizo kadhaa kuhusu mumewe ambayo yalijifunua punde alipojitosa kwenye ndoa hiyo.

Kabla ya kuoelewa nilikuwa na matarajio mengi kuwa tungeelewana na mume wangu. Lakini inatokea kila siku ni kelele. Alikuwa anakasirika sana. Kabla ya kupata mimba, hata mimi nilikuwa nakasirika namjibu," Kawira alisema.

Alifichua kuwa yeye na mumewe walichumbiana kwa takriban miaka miwili kabla ya kufanya harusi ya kanisa. Katika kipindi hicho cha kuchumbiana, muigizaji huyo hakuwahi kuenda nyumbani kwa mumewe bila kuandamana na mtu mwingine.

"Nilifanya harusi ya kanisa. Nilikuwa bikra nikienda kuolewa.  Nilikuwa nimeenda kwake mara mbili tu na lazima kulikuwa na mtu wa kuandamana naye. Hata hatukuwahi busu," alisema.

Kawira alisema ilifika muda akaona kama kwamba yupo pekee yake katika ndoa hiyo. Alidokeza kuwa hakuna ushauri wake wowote ambao mumewe angechukua.

Licha ya ndoa yake kujaa masaibu chungu nzima, hakuwahi kueleza yeyote kuhusu mambo aliyokuwa akiyapitia.

"Ni mambo ambayo yalianza kutoka kwa uwanja wa harusi. Singetoka mara moja. Nilidhani ni woga tu. Nilidhani niliogopa zaidi kwa kuwa sikulelewa na baba. Alifariki nikiwa na miaka minne," alisimulia.

Alifichua kuwa kabla ya kufanya maamuzi ya  kugura ndoa hiyo kabisa, alikuwa ameondoka na kurudi tena mara mbili.

Miaka miwili na miezi minne imepita tangu atoroke.