Wafula ataka kupatanishwa na mwanamke wa ndoa ya mwezi mmoja akiwa na watoto 3

Wafula alisema alioa mwanamke huyo akiwa na watoto 3 na waliishi pamoja chini ya mwezi mmoja tu.

Muhtasari

• Jedidah alisema kuwa aliahirisha kuolewa baada ya kuona kuwa anamtesa mtoto wake anayeingia darasa la 8.

• Pia alisema hofu kuu ilikuwa kwa wazazi wake Wafula kumkubali na watoto ambao si wa ukoo wao.

GHOST NA GIDI STUDIONI
GHOST NA GIDI STUDIONI GHOST NA GIDI STUDIONI
Image: RADIO JAMBO

Katika kitengo cha Patanisho kwenye kituo cha Radio Jambo asubuhi ya Jumatatu, mwanamume kwa jina Kelvin Wafula alitaka kupatanishwa na mwanadada ambaye alisema walikuwa wameoana kwa kipindi kifupi.

Wafula alisema kwamba alikuwa ameishi na mwanadada huyo, mama wa watoto watatu chini ya mwezi mmoja tu.

Jedidah, Mama huyo wa watoto watatu alikuwa anafanya kazi Nairobi na baada ya kuunganishwa na Wafula kupitia kwa shemeji yake, walizungumza na kuelewana kwamba mwanadada huyo atoke Nairobi alikokuwa akifanya kazi na kusafiri hadi Kitale kwa kina Wafula.

Wafula alimrai Jedidah mara kadhaa kuacha kazi yake Nairobi na kuenda Kitale ili kuishi naye kama wanandoa na kuahidi kulea watoto wake wote watatu, huku akimwambia kwamba alikuwa radhi kumpeleka mtoto mkubwa kuingia shule darasa la 8.

Katika watoto hao wote watatu wa Jedidah, hakuna hata mmoja ambaye alizaa na Wafula.

“Kitale ndio mara ya kwanza kukutana, tulikaa karibu mwezi.. hakuwa mke wangu ndio tulikuwa tunapanga kuoana. Alikuwa ameoleka na akakosana na huyo mtu, ana watoto watatu na sijapata mtoto na yeye. Mtoto mkubwa alikuwa aende darasa la 8,” Wafula alisema.

Mwanamume huyo alisema baada ya kuishi kutoka Januari, alienda kazini na siku moja kurudi kwa chakula cha mchana, akampata Jedidah hayuko. Kumtafuta kwa simu akamwambia alirudi Nairobi alikokuwa akifanya kazi, yeye akifikiria alikuwa ameendea mtoto mkubwa.

Kwa upande wake Jedidah, alisema kwamba aliamua kughairi kuolewa kwa kile alisema ni kuona watoto wake watateseka na pia kuhofia jinsi familia ya Wafula itamchukulia na watoto watatu ambao si wa ukoo wao.

“Tulikuwa tumepanga na nikaona mtoto anaenda darasa la 8 na nikaona nikiamua kuoleka mtoto ataumia. Nilimueleza sijamficha lolote. Nimekaa bila mume kwa miaka 2. Nilikaa chini nikaona watoto wangu wataumia. Mimi naogopa wazazi wake huenda hawatanikubali na watoto wangu ila nampenda,” Jedidah alisema.

Gidi alimshauri Wafula kutomuita Jedidah kama mke wake kwani hawakuwa wameishi naye kwa siku nyingi, huku pia akionesha wasiwasi wake kwa Wafula kusema anataka kuwalea watoto wa Jedidah pasi na kazi maalum.