Patanisho: Jamaa aliyemuoa dada mdogo wa mke wa kakake atoroka saa nane usiku kimyakimya

"Kuna wakati alianza kunitusi akiniambia hatawahi kuniita shemeji" Jane alilalamika.

Muhtasari

•Jane alisema Douglas alikuwa amemtembelea pamoja na mke wake, ambaye pia ni dadake ila wakaondoka ghafla bila taarifa yoyote.

•Douglas alipopigiwa simu aliweka wazi kwamba hana ugomvi wowote na shemejiye wala ndugu yake mkubwa.

Ghost na Gidi
Ghost na Gidi
Image: RADIO JAMBO

Jumatatu asubuhi, Jane Nasimiyu ,27, kutoka Kitale alituma ujumbe akiomba kupatanishwa na shemeji yake Douglas Mulango ,22, ambaye alikosana naye wiki jana. 

Jane alisema Douglas alikuwa amemtembelea pamoja na mke wake, ambaye pia ni dadake ila wakaondoka ghafla bila taarifa yoyote.

"Niliwakaribisha kwangu alafu wakaondoka saa nane ya usiku wakaenda. Hakuna kitu ambacho tuliwafanyia. Mzee wangu ni ndugu wa huyo jamaa, ndugu yake mkubwa amenioa, tena ameoa dada yangu," Jane alisema.

Aliongeza, "Kuna wakati alianza kunitusi akiniambia hatawahi kuniita shemeji. Sasa wananitumia meseji wakisema mara wako kwa marafiki. Ningetaka aniambie kama nilikosea mahali fulani niombe msamaha."

Douglas alipopigiwa simu aliweka wazi kwamba hana ugomvi wowote na shemejiye wala ndugu yake mkubwa.

"Mimi nilioondoka tu hakuna mahali mlinikosea. Mimi nikijaribu kutuma meseji hunijibu. Nilikaa nyumbani nikaona nakosa amani ya akili ikabidi niende niangilie vile mambo itakuwa sawa. Saai niko Western," alisema.

Douglas alibainisha hana kinyongo dhidi ya Jane na mumewe ila akalalamika kuwa kila anapowatumia meseji hawajibu.

Aidha, alikana madai ya Jane kuwa aliondoka saa nane usiku.

"Haikuwa saa nane, ilikuwa saa kumi na moja. Nilikua nimeongea na kakangu nikamwambia nasafiri," alisema.

Aliendelea, "Niliamka saa kumi nikaanza kujitayarisha. Nilitoka nikaangalia gari ambayo ingeweza kunifikisha Western nikaenda. Mimi sina ubaya na mtu yeyote."

Jane alikiri kuridhishwa na patanisho yake na shemejiye na akamhakishia kwamba yupo tayari kumsaidia kila anapokwama.

Douglas kwa upande wake alimhakikishia shemejiye kuwa yupo sawa ila anahitaji amani na utulivu wa akili.