Patanisho: Mwanadada alalamikia kutelekezwa na mumewe kijijini, kuomba msamaha miaka 3 bila mafanikio

"Nikitafuta number nyingine anablacklist. Aliniforce nizae na yeye. Baada ya kuzaa akanitupa hivyo," Priscilla alilalamika.

Muhtasari

•Priscilla alisema ndoa yao ya miaka miwili ilianza kusambaratika baada ya mumewe kumtuma nyumbani kwao kisha kukatiza mazungumzo. 

•Alieleza kwamba alipitia masaibu mengi kule nyumbani kwa kina Opama hadi akalazimika kuondoka na kumuacha mwanawe.

Ghost na Gidi
Ghost na Gidi
Image: RADIO JAMBO

Priscilla Shegera ,24, kutoka Teso alituma ujumbe akiomba kupatanishwa na aliyekuwa mume wake Alex Opama ,31, ambaye alitengana naye Oktoba  2021.

Priscilla alisema ndoa yao ya miaka miwili ilianza kusambaratika baada ya mumewe kumtuma nyumbani kwao kisha kukatiza mazungumzo. Wawili hao walikuwa na mtoto mmoja pamoja kabla ya kutengana.

"Alinituma niende kwao na mtoto. Kufika kwao, hakunipigia simu. Alimpigia tu mama yake akamuuliza kama hao watu wamefika salama, akasema tumefika saa hiyo kisha  akakata simu," Priscilla alisimulia.

Priscilla alisema mumewe aliendelea kusalia kimya kwake na hawakuweza kuzungumza kwenye simu kila alipompigia.

"Baada ya wiki moja nilimpigia simu akakata. Siku ingine nikampigia simu usiku nikasikia ako bize, nikafikiria yuko kazini. Mwezi ukaisha kama mtu haniongeleshi," alisema.

Alieleza kwamba alipitia masaibu mengi kule nyumbani kwa kina Opama hadi akalazimika kuondoka na kumuacha mwanawe.

"Jamaa akituma pesa alikuwa anatumia mamake  na mimi ndiye naumia na mtoto. Kama ni sabuni, alikuwa anatumia mamake ananikatia kipande kidogo anasema ikiisha nijipange. Niliachia mtoto wake na mama yake," alisema.

Aliendelea, "Sasa hivi ameniblacklist. Nikitafuta number nyingine anablacklist. Aliniforce nizae na yeye. Baada ya kuzaa akanitupa hivyo."

Juhudi za kuwapatanisha wawili hazikufua dafu kwa kuwa Alex hakuchukua simu licha ya Gidi kumpigia mara kadhaa.

Priscilla alisema, "Namtafuta kwa sababu ako na mtoto wangu. Nilimwambia mama mkwe anipatie mtoto akakataa. Mama alitaka niondoke ndiyo kijana wake aendelee kutuma pesa kwake."

Alipopatiwa nafasi ya kuzungumza na Alex hewani alisema, "Alex nakupenda naomba turudiane. Kama nilikukosea naomba msamaha. Nimeomba mara nyingi na hutaki kunisamehe... Nilianza kuomba msamaha 2021 lakini hataki kunisamehe."

Je, una ushauri gani kwa Bi Priscilla?