Patanisho: Kondoo asababisha msukasuko mkubwa katika ndoa ya miaka 3

Kiplangat alidai mkewe alitaka kumuuza kondoo huyo ili kutoroka kwenda Nairobi.

Muhtasari

•Eunice alieleza kwamba hajatengana na mumewe ila fitina za mama mkwe zimesababisha misukosuko ndani ya ndoa yao ya miaka mitatu.

•Eunice alimshtumu mumewe kwa kumpiga, madai ambayo alikubali na kujitetea kuwa, "Ni lazima unaweka discipline kidogo, sasa kama mtu amekuita mjinga..," 

Gidi na Ghost
Gidi na Ghost
Image: RADIO JAMBO

Jumatatu asubuhi, Eunice Khavayi almaarufu Mama Migel ,22, kutoka Trans Nzoia alituma ujumbe akiomba kupatanishwa na mume wake Edwin Kiplangat ,26.

Eunice alieleza kwamba hajatengana na mumewe ila fitina za mama mkwe zimesababisha misukosuko ndani ya ndoa yao ya miaka mitatu.

"Naomba nipate kujua ukweli wa mzee, sikai na yeye lakini akitoka kazi anaambiwa fitina na mama mkwe. Saa hii sina amani na yeye nikimpigia simu hashiki, tafadhali mnisaidie nijue msimamo wake," Eunice aliomba.

Eunice alidai kwamba mumewe alimuuza kondoo ambaye alikuwa amenunua baada ya kupewa maneno ya fitina na mamake.

"Nilikuwa mgonjwa. Nikakaa wiki moja nikaenda hospitali. Nilimwita kutoka kazini ili aje anipeleke hospitali. Alipitia kwao sijui mamake alimwambia nini. Nilikuwa nimenunua kondoo, akaja akauza Sielewi kwa nini na alikuwa ameshika mshahara juzi. Mama yake alimwambia nataka kuuza huyo kondoo nitoroke. Alimwambia mambo mingi, anasema eti ameambiwa nataka kutoroka.Nataka nijue ukweli wake," alisema Eunice.

Kiplangat alipopigiwa simu aliweka wazi kwamba hana shida yoyote na mkewe ila akamshtumu kwa 'kushindwa kuongea.'

"Ata hakuna shida.  Yeye hajui kuongea. Juzi vile aligonjeka, nilikuwa kazini nikatoka kuenda kumuona. Ni kweli nilishika kondoo nikauza. Kuna rafiki yangu ambaye pia alileta bibi yake kutoka Nairobi. (Eunice) Walikuwa wanazungumza na yeye watoroke waende watafute kazi Nairobi," Kiplangat alisema.

Eunice alimshtumu mumewe kwa kumpiga, madai ambayo alikubali na kujitetea kuwa, "Ni lazima unaweka discipline kidogo, sasa kama mtu amekuita mjinga..," 

Kiplangat hata hivyo alikubali kuzungumza na mkewe baadaye ili kusuluhisha mzozo wao.

"Nitampigia simu tuongee na yeye..Nitakuja nyumbani tutangoea," alimwambia Eunice.

Eunice alimhakikishia mumewe kwamba hana shida naye ila akamuomba kujiepusha na fitina za watu.