Patanisho: Mwanadada ajawa wasiwasi baada ya mumewe polisi kumnyamazia kwa saa 12

"Huwa ananishuku, haniamini, na anajua mimi ni mtu nampenda. Aniambie shida ni nini.Kama tuko wawili nikae nikijua ," Sheila alisema.

Muhtasari

•Sheila alisema ndoa yake ya miaka mitatu ilianza kuyumba takriban miezi miwili iliyopita baada ya tabia za mumewe kuanza kubadilika ghafla.

•Sheila alidokeza kuwa hivi majuzi kumekuwa na kutoaminiana katika ndoa yao, jambo ambalo huenda limechangia matatizo yao.

Gidi na Ghost
Image: RADIO JAMBO

Katika Patanisho, Sheila kutoka Kitengela alituma ujumbe akiomba kupatanishwa na mumewe Vincent ambaye hajakuwa na maelewano mazuri naye.

Sheila alisema ndoa yake ya miaka mitatu ilianza kuyumba takriban miezi miwili iliyopita baada ya tabia za mumewe kuanza kubadilika ghafla.

"Tuko pamoja lakini siku kama tatu zimepita hatuongeleshani. Tumekuwa na masuala. Huwa anafanya kazi Garissa na mimi niko Kitengela. Kumekuwa na masuala kidogo, akikuja nyumbani ni kama hana haja na mimi," Sheila alisimulia.

Aliendelea, "Nilijaribu kuongea na wazazi wake na mabinamu zake. Imefika mahali nataka tu kujua tu msimamo wake. Inaweza kuwa amechoka na mimi na haniambii, kama hanitaki ni sawa mimi naweza kuenda. Alinioa na mtoto mmoja na tumepata mmoja naye. Tulikuja jijini Nairobi mwezi wa wa kumi na moja, alianza kubadilika miezi kama miwili iliyopita. Nilijaribu kuongea na wazazi wake waone shida ni nini lakini hasemi. Wakati akija nyumbani anakuwa amebadilika na anakuja ananipiga."

Vincent alipopigiwa simu, alipuuzilia mbali madai ya kukatiza mawasiliano na mkewe na kubainisha wamekuwa wakiongea.

Sheila hata hivyo alilisitiza kwamba wamekuwa wakigombana na kumtaka mumewe kuweka msimamo wake wazi.

"Tatizo ni gani? Ni hupatiwi chakula ama ni nini? Mimi bado ninampenda na hata jana nilimpigia simu tukaongea. Sina mtu mwingine. Ajue hivyo vitu anafikiria havipo. Ni ile akinikasirisha simzungumzii," alisema Vincent.

Sheila alidokeza kuwa hivi majuzi kumekuwa na kutoaminiana katika ndoa yao, jambo ambalo huenda limechangia matatizo yao.

"Tumekaa na yeye muda mrefu huwezi kusema sijui akibadilika. Huwa ananishuku, haniamini, na anajua mimi ni mtu nampenda. Aniambie shida ni nini.Kama tuko wawili nikae nikijua  ," alisema.

Vincent alisema, "Bado nampenda, lakini hiyo ishu ya kudanganya na tumeongea na yeye aache. Tumekaa na yeye sana aseme kama amewahi kuniona na mtu, huwa anashinda na simu yangu. Hakuna mtu, ni yeye tu. Akae akijua hizo vitu anafikiria hakuna,"

Wakati alipopewa nafasi ya kumuambia mumewe maneno ya mwisho hewani, Sheila alisema, "Tumetoka mbali na wewe. Nakupenda na wewe ndo mume wangu wa maisha."

Vincent kwa upande wake alisema, "Sheila  wewe jua bwanako vile anakuwa wakati amekasirika.  Ukiona nimenyamaza jua tu ni hasira. Nitajaribu kubadilika lakini. Nakupenda. Hakuna kitu ingine umenikosea. Ni kuongea tu, mazungumzo."